(1) Kufahamu kwa nini kujifunza Biblia kwa kina ni muhimu kwa mkristo.
(2) Kuwa na uwezo wa kutaja hatua tatu muhimu za kujifunza Biblia.
(3) Anza mchakato wa kujifunza kwa umakini kifungu cha andiko kilichochaguliwa.
(4) Kutambua umuhimu wa kuangaziwa na Roho Mtakatifu kwa ajili ya kutafsiri Biblia.
Utangulizi
Moja ya kusudi ya kozi hii ni kukusaidia kukua katika ujifunzaji wako binafsi na matumizi ya Maandiko. Hatua ya kwanza ni kutathmini kwa uaminifu mwenendo wako wa sasa wa usomaji wa Biblia.
► Chukua dakika kadhaa kujadili mwenendo wako wa sasa wa usomaji wa Biblia. Huu si wakati wa kukosoana; ni wakati wa kutafakari juu ya swali, “Ni kwa namna gani ninasoma Neno la Mungu?” Haya hapa ni maswali ya kutafakari:
Ni mara mara nyingi kiasi gani ninasoma Biblia?
Ninaposoma Biblia, ninatumia muda kiasi gani?
Ni kwa namna gani ninachagua kifungu cha kusoma?
Je, ninaelewa kile ninachokisoma?
Je, ninakumbuka ninachokisoma?
Je, ninaweza kutumia katika Maisha yangu?
Ni sababu gani 2-3 zinazonifanya nisisome Biblia zaidi ya ninavyosoma sasa?
Tinghao, ni mkristo wa Taiwani, amekuwa mkristo wa miaka 15, lakini anaonesha viashiria vichache vya ukuaji wa kiroho. Huku kukosa ukuaji wa kiroho kulimsumbua sana. Baada ya ibada ya jumapili, masumbufu yake yalikuwa wazi. “Mchungaji, unaniambia kusoma Biblia. Unasema kwamba Mungu atazungumza na mimi kupitia neno lake. Nimekuwa nikijaribu kusoma kila asubuhi, na halisemi chochote kwangu. Shida ni nini?”
Mchungaji akajibu, “Tinghao, niambie unasoma Biblia kwa namna gani.” Majibu ya Tinghao yalionesha jambo muhimu sana katika masumbufu yake. Alijibu, “Kila asubuhi kabla ya kazi, ninafungua Biblia na ninasoma mstari.” Mchungaji akafuata, “Je, unasoma kitabu chote cha Biblia au hata kumaliza sura moja kabla ya kuendelea?” “Hapana, Ninasoma tu mstari mmoja kila asubuhi – popote pale ambapo Biblia yangu itafunukia. Na haijanisaidia sana!”
Ili kumsaidia Tinghao kuelewa tatizo la kusoma Biblia kwa mtindo wake, mchungaji alimuomba afungue Biblia na kusoma mstari wa kwanza aliouona. Tinghao akasoma, “Na watu wa Negebu wataumiliki mlima wa Esau; na watu wa Shefela watawamiliki Wafilisti; nao watalimiliki konde la Efraimu, na konde la Samaria, na Benyamini atamiliki Gileadi” (Obadia 1:19).
Kisha mchungaji akamuuliza Tinghao maswali kadhaa. “Negebu ni wapi? Shefela ni wapi? Wapi ni nchi ya Efraimu? Samaria? Benyamini? Gileadi?” Jibu kwa kila swali lilikuwa ni “Sifahamu.” Juma lililofuata walianza kujifunza Biblia juu ya “Namna ya kusoma Biblia.” Katika majuma kadhaa, Tinghao alianza kujifunza kanuni kadhaa za kutafsiri Biblia. Alijifunza kuelewa ni kwa jinsi gani Maandiko yanazungumza na sisi leo.
Lengo la kozi hii ni ili kukusaidia kujifunza na kutendea kazi kanuni za msingi za kutafsiri Biblia. Kupitia masomo na mazoezi haya, utapata nyenzo za kukusaidia kulielewa Neno la Mungu, kulitumia katika maisha yako, na kuwafundisha wengine.
Kwa nini nijifunze Biblia?
Baadhi ya watu wanakwepa kusoma Biblia kwa sababu wanaamini ni ngumu kuielewa. Wengi wa wanaoamini kwamba Biblia ni neno la Mungu hawafahamu namna ya kuitafsiri na kuitumia. Kujifunza Biblia ni kazi ngumu. Je, inastahili kazi hiyo? Kwa nini tujifunze Biblia?
Mungu Amejifunua Mwenywe Kupitia Maandiko
Maandiko yanatuonesha sisi Mungu ni nani. Neno la Mungu ni maelezo ya asili ya Mungu (Zaburi 119:15, 27). Maandiko yanatuonesha sisi ni namna gani Mungu anafikiri, nini ni muhimu kwake, ni kwa namna gani anahusiana na watu, na ni kwa namna gani ametenda katika historia ya mwanadamu. Sheria ya Mungu (kile anachohitaji) kinaakisi sifa zake, haki yake, na hekima yake (Zaburi 119:137). Kila wakati tunaposoma Biblia, tunatakiwa kuweka umakini wetu kwenye kile inachoonesha kuhusu Mungu.
Maandiko yanamuonesha Mungu kwa anayeabudu. Pia yanaongoza mwitikio wa anayeabudu kwa Mungu, yakionesha namna tunayotakiwa kuishi.
Biblia ni Taa
Mzaburi analilinganisha Neno la Mungu na taa ambayo inaongoza njia ya namna ya kuishi (Zaburi 119:105). Biblia ni kweli ya Mungu inayotufundisha sisi namna ya kufikiri na kuishi.
► Soma Zaburi 19:7-11, Zaburi 119:160, na 2 Timotheo 3:16-17.
Neno la Mungu ni chanzo cha mafundisho sahihi. Biblia ina maarifa yote yanayohitajika kwa ajili ya wokovu na utakatifu. Kanuni hii haimaanishi kwamba tunaweza kuelewa kila kitu katika maandiko bila msaada mwingine. Haimaanishi kwamba tamaduni si za muhimu. Inamaanisha kwamba Neno la Mungu ni mamlaka ya mwisho kwa mwamini.
Kwa sababu Neno la Mungu ni chanzo cha kweli, maarifa ya maandiko yanatuandaa na kututengeneza sisi kwa huduma. Tunapolifundisha Neno la Mungu kwa usahihi, tunafundisha kwa mamlaka ya Mungu. Kweli ni yake, sio yetu.
Biblia ni maziwa ya kiroho
Petro alisema kwamba tunapaswa kuitamani Biblia kwa kiwango kile ambacho mtoto anayatamani maziwa (1 Petro 2:2). Kama vile ambayo mtoto anayahitaji maziwa ili kukua kimwili, mkristo anatakiwa kuwa na Maandiko ili kukua kiroho. Pasipo kuwa na mlo wa mara kwa mara wa Neno la Mungu, hatutakua kiroho.
Tunapojifunza stadi za kutafsiri Biblia na kufanya mazoezi ya kung’amua kweli ya Mungu kutoka katika Neno la Mungu, tunakua (Waebrania 5:14). Uwezo wetu wa kutumia Neno la Mungu kufundisha wengine utakua.
Biblia ni asali tamu
Mzaburi analinganisha Neno la Mungu na asali (Zaburi 19:10, Zaburi 119:103). Asali ni tamu na yenye afya. Tunatakiwa kufurahia kujifunza Neno la Mungu, na si kuona kuwa ni kazi isiyovutia. Kama vile tu mwanajeshi aliye vitani anavyofurahia kusoma barua iliyotoka nyumbani, tunatakiwa kufurahia tunaposoma Biblia, barua ya Mungu kwa watoto wake.
Kijana wa kiyahudi alianza shule ili kwamba aweze kujifunza kusoma sheria, mwalimu aliweka asali katika herufi za kwanza za silabi na mtoto angejitahidi kulamba ukurasa ili aonje utamu wa asali. Mwalimu alitumia somo hili la vitu akitarajia kwamba “mtoto atajifunza kuhusianisha [sheria] na Furaha na ladha njema.”[1]
Biblia ni upanga wa Roho
Neno la Mungu ni silaha yetu katika vita za kiroho (Waefeso 6:17). Yesu alipata majaribu kule nyikani, aliyajibu mashambulizi ya Shetani kwa kunukuu kutoka Kumbukumbu la Torati (Mathayo 4:1-11).
Maandiko yanatutia nguvu kwa ajili ya ushindi wa kiroho na huduma yenye ufanisi. Kupitia kujifunza Biblia, tunaandaliwa kwa ajili ya kupinga mafundisho potofu, ili kulikuza kundi letu katika mafundisho sahihi, na kuhudumu kwa ufanisi katika ulimwengu wa sasa.
Sababu zisizo sahihi za kujifunza Maandiko
► Soma Waebrania 4:12-13.
Zipo sababu nzuri sana za kujifunza Maandiko, lakini kuna wakati watu wanasoma au wanajifunza Maandiko wakiwa na msukumo mbaya.
Baadhi ya watu wanaweza kujifunza Maandiko ili tu kukusanya ushahidi ili kutetea hoja au mawazo yao. Pengine hata wanataka kutumia ufahamu huo ili kuwadhibiti wengine chini ya ushawishi wao.
Baadhi ya watu wanajifunza Maandiko kwa sababu za kiburi. Pengine wanafikiri watapata vyeo vya kiroho na kuwa juu ya watu wengine. Pengine wanapenda watu wengine wawafikirie na wawasifu kwa mafanikio yao. Au pengine wanafikiri kwamba kujifunza Maandiko kutawafanya wao kupata upendeleo kwa Mungu.
Hizi zote ni sababu zisizo sahihi za kusoma au kujifunza Neno la Mungu. Waebrania 4:12-13 inaonesha nia njema kuhusiana na Maandiko. Badala ya kutumia Maandiko ili kukamilisha malengo binafsi, tunatakiwa kukumbuka kwamba hili ni Neno la Mungu, na si letu. Tunatakiwa kujifunza tukiwa na mtazamo wa kumuheshimu Mungu. Biblia ni mamlaka yetu, na tunatakiwa tuitii. Tunapolifundisha kwa wengine, tunatakiwa kufanya hivyo kwa unyenyekevu.
Tunapojifunza na kulifundisha Neno la Mungu kwa namna hii, litafunua dhambi na makosa katika maisha yetu na kutuonesha namna ya kuacha. Litabadilisha maisha yetu na maisha ya wale tunaowatumikia na kuwaongoza.
► Ni mchakato gani ambao unautumia kwa sasa unapojifunza kifungu cha maandiko? Jadili hatua mahususi ambazo unachukua ili kupata maana ya andiko la Biblia.
Tinghao anakubali kwamba kujifunza Biblia ni muhimu. Hata hivyo, hakujua namna ya kujifunza maandiko. Alihitaji njia.
Kozi hii inakusudia kupata njia kwa ajili ya ujifunzaji wa Biblia wenye ufanisi. Wachungaji wanaweza kutumia hatua hizi tatu katika maandalizi ya ujumbe. Waalimu wa Biblia wanaweza kutumia hatua hizi kuandaa masomo ya Biblia. Kila mwamini anaweza kunufaika na kutumia njia hii kwa ajili ya kukua kiroho kibinafsi.
Njia inayofuatwa na kozi hii inahusisha hatua tatu.
Uchunguzi
Katika hatua hii, tunajiuliza, “Ninaona nini katika Biblia?” katika hatua hii, tunachunguza taarifa nyingi kwa kadiri inavyowezekana kuhusiana na Maandiko. Wasomaji wengi huruka hatua ya Uchunguzi na kwenda moja kwa moja katika tafsiri. Hatuwezi kuelewa Maandiko kikamilifu hadi tumechunguza nini yanasema. Katika mchakato wa Uchunguzi, tunaangalia katika taarifa za ndani za andiko lenyewe. Tutajifunza kutambua taarifa ambazo ni muhimu katika andiko. Mahususi kabisa, tutajifunza maneno, muundo, aina ya fasihi, na mazingira.
Maneno
Tunapojifunza kitabu cha Biblia, tunaangalia maneno ambayo yametumika mara kadhaa katika kitabu chote. 1 Yohana inatumia namna mbalimbali ya neno kujua zaidi ya mara 30 katika sura 5. Unaposoma waraka wa Yohana, unaweza kuanza kwa kulifuatilia neno hili katika kitabu. Orodha ya mahali ambapo Yohana amelitumia neno hili itatusaidia sisi kuanza kutafsiri ujumbe wake. Ili kuelewa ujumbe wa Yohana, tunaweza kuuliza, “Yohana anasema tunaweza kujua nini?” na “Zipi ni sifa za wale wanaojua?”
Muundo
Vitabu vya Biblia vimetengenezwa kwa umakini sana chini ya uvuvio wa Roho Mtakatifu. Unaposoma kitabu kama Injili ya Yohana, utaweza kuona kwamba, Yohana ameipanga Injili yake katika alama saba ambazo zinamuonesha Yesu ni nani. Tunapochunguza muundo wa kitabu, unatupa sisi uelewa mzuri wa kusudi la Yohana.
Tunaposoma kifungu cha Maandiko, tunaweza kuona kwamba muundo unafuata habari (kama katika Luka 9:28-36). Kinaweza kutupa sababu ya kuhitimisha (kama katika Warumi 6:1-13). Unaweza kutumia taarifa kutupa orodha ya dondoo (kama katika Waefeso 6:13-18). Pia kuna aina nyingine ya muundo.
Aina ya Fasihi
Paulo aliandika nyaraka zilizopangwa vizuri sana ambazo zilitoa hoja zake kama ambavyo mwanasheria anajenga hoja zake kuelekea juu kileleni kwenye dondoo kuu. Ili kusoma vizuri Warumi au nyaraka nyingine, unatakiwa kufuata mtiririko wa mawazo wa Paulo.
Kinyume chake, Yona ni habari fupi ya kihistoria iliyoandikwa ili kuelezea upendo wa Mungu kwa watu wote. Ili kukisoma vizuri, lazima uulize, “Ni kitu gani kinaifanya habari hii kuwa ya kushangaza, na isiyo ya kawaida?” Hapa sasa unakuwa tayari kutafsiri kitabu cha Yona kwa kuuliza, “Taarifa za kina za habari hii zinamaanisha nini?”
Mazingira
Hapa tunauliza maswali kama, “Paulo alikuwa wapi alipoandika waraka kwa Wafilipi akiwa na ujumbe wake wa furaha?” alikuwa Rumi, akingojea kesi yake na inawezekana akingojea hukumu yake ya kifo. Mazingira yanatufanya tuangalie sababu za Paulo kusema alikuwa na furaha, kwa sababu alikuwa na furaha hata kama binafsi alikuwa katika hali mbaya.
“Yohana alikuwa wapi wakati mbingu zinafunguka kufunua mpango wa Mungu wa milele katika kitabu cha Ufunuo?” alikuwa uhamishoni katika kisiwa cha Patimo. Kipindi cha mateso makali kilifanya ujumbe wa ushindi wa Mungu kuwa wa kutia moyo katika Imani.
Tafsiri
Katika hatua hii, tunauliza, “Biblia inamaanisha nini?” Baada ya kuwa tumekusanya taarifa nyingi za Uchunguzi kwa kadiri inavyowezekana, tunauangalia ujumbe wa maandiko. Tutajifunza kutafuta mada kuu ambayo inaunganisha kitabu pamoja na ujumbe wa sura na mistari husika. tutauliza, “upi ni ujumbe wa kitabu hiki kwa wapokeaji wa kwanza?” Tutatafuta kanuni ambazo ni kweli kwa nyakati zote, mahali pote, na tamaduni zote.
Matumizi
Katika hatua hii, tunauliza, “Ni kwa namna gani ninaitumia Biblia katika maisha na huduma leo?” Haitoshi tu kuelewa maana pasipo kuitendea kazi katika maisha yetu.
Katika kitabu chake, Howard Hendricks anashauri maswali mawili kuhusiana na matumizi:[1]
1. Inafanyaje kazi kwangu? Hii inaangazia matumizi ya andiko katika maisha yangu.
2. Inafanyaje kazi kwa wengine? Hii inaangazia matumizi ya andiko katika maisha ya wale ambao ninawaahudumia.
Kule Uingereza kuna mhadhiri wa chuo kikuu ambaye ni msomi anaheshimika sana wa historia ya kanisa. Kitaaluma, anaifahamu Biblia vizuri sana; kibinafsi, anakana Imani yeyote kuhusiana na Mungu na neno la Mungu. Mtu huyu anafahamu vizuri kuhusiana na Uchunguzi na tafsiri. Kwa bahati mbaya, hajawahi kutumia kweli ya maandiko katika maisha yake.
Yakobo anamuelezea mtu wa aina hii kama hivi: “Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo” (Yakobo 1:23-24). Mhadhiri kule Uingereza ni kisa cha juu sana; hata hivyo, wapo watu wengi sana ambao wanafahamu maandiko yanasema nini, lakini wanashindwa kuyaishi katika maisha yao ya kila siku. Ujifunzaji wa kweli wa Biblia unatakiwa kupelekea katika kutendea kazi kivitendo.
[1]Howard G. Hendricks and William D. Hendricks, Living by the Book (Chicago: Moody Publishers, 2007)
Kazi ya Roho Mtakatifu katika Tafsiri
► Je, mwamini anaweza kuelewa maana ya maandiko?
Jibu la swali hili ni “ndiyo, lakini kwa kiasi tu.” Katika kozi hii, tunajifunza mchakato wa kutuongoza katika tafsiri zetu. Hatua hizi zitatusaidia kuelewa ujumbe wa neno la Mungu. Biblia, kusoma kama vitabu vingine, kutafunua kweli nyingi kwa msomaji yeyote.
Hata hivyo, bila kuangaziwa na Roho Mtakatifu, uelewa wa mtu utakuwa finyu. Usomaji wa kitaaluma pekee kamwe hauwezi kufunua kweli ya Kiroho. Paulo anaandika:
Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu. Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni (1 Wakorintho 2:11-14).
Asiyeamini anaweza kuelewa baadhi ya ujumbe wa andiko, lakini kweli za ndani za Biblia zinafunuliwa kupitia kuangaziwa na Roho Mtakatifu. Kusoma maandiko ni zaidi ya kupata taarifa; inahitaji imani na utii. Ni hadi tutakapojitia katika mamlaka ya Neno la Mungu, Roho wa Mungu hataweza kufanya kazi hii ya kutubadilisha katika maisha yetu. Kwa sababu hii:
1. Kujifunza kwetu kunatakiwa kutanguliwa na maombi. Tunatakiwa kumuuliza Roho Mtakatifu kutuongoza katika kujifunza kwetu. Yakobo anaandika, “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa” (Yakobo 1:5).
2. Ujifunzaji wetu wa Maandiko unatakiwa kufuatwa na mwitikio binafsi. Lengo la kujifunza Biblia ni zaidi ya uelewa wa kiakili wa kupata taarifa; lengo ni kubadilishwa kibinafsi. Kama hatutabadilishwa kupitia kujifunza kwetu, tumekosa kusudi la kujifunza. Badiliko linakuja tu kupitia Roho Mtakatifu.
Katika mfano wa Yesu kuhusiana na mpanzi na mbegu. Baadhi ya mbegu zilianguka njiani na zililiwa na ndege. Mbegu nyingine hazikuwa na mizizi zikafa jua lilipokuwa kali. Mbegu nyingine zilisongwa na miiba. Lakini mbegu nyingine zilianguka katika udongo mzuri na kuzaa matunda. Yesu alielezea kwamba udongo mzuri ni yule mtu ambaye analisikia neno la Mungu na kulielewa (Mathayo 13:3-23). Mfano huu unaonesha kwamba inawezekana kulisikia neno la Mungu pasipo kulielewa. Tunalielewa neno la Mungu vema endapo tu tutaiweka wazi mioyo yetu kwa sauti ya Roho Mtakatifu.
(2) Zipo hatua tatu katika mchakato wa kujifunza Biblia.
Uchunguzi: Ninaona nini katika Biblia? Jifunze:
Maneno
Muundo
Aina ya Fasihi
Mazingira
Tafsiri: Biblia inamaanisha nini?
Matumizi: Ni kwa namna gani ninaitumia Biblia katika maisha na huduma leo? Uliza:
Inafanyaje kazi kwangu?
Inafanyaje kazi kwa wengine?
(3) Tunatakiwa kuangaziwa na Roho Mtakatifu wakati tunajifunza Biblia. Kwa sababu hii
Kujifunza kwetu kunatakiwa kutanguliwa na maombi.
Ujifunzaji wetu wa Maandiko unatakiwa kufuatwa na mwitikio binafsi.
Somo la 1 Zoezi
Kwa kuanza mchakato wa kutafsiri, chagua kifungu kimojawapo kati ya vinavyofuata.
Kumbukumbu la Torati 6:1-9
Yoshua 1:1-9
Mathayo 6:25-34
Waefeso 3:14-21
Wakolosai 3:1-16
Utajifunza Maandiko haya wakati wote wa kozi. Kwa somo hili la kwanza, soma maandiko kwa umakini. Tengeneza nakili katika maeneo matatu:
1. Uchunguzi: Orodhesha taarifa nyingi kwa kadiri unavyoweza kuhusiana na andiko ulilochagua. Kwa kutegemea andiko, taarifa zenu zitatofautiana. Baadhi ya maswali ambayo yatakusaidia ni haya:
Matukio yaliyonakiliwa katika andiko hili yalifanyika wapi?
Nani ni wahusika katika andiko hili?
Andiko hili linaagiza nini?
Ni maneno gani ambayo yanarudiwa rudiwa katika andiko hili?
2. Tafsiri: Katika sentensi 2-3, fupisha ujumbe wa kifungu cha maandiko.
3. Matumizi: Orodhesha njia 2-3 ambazo unaweza kutumia andiko hili katika maisha na huduma yako.
SGC exists to equip rising Christian leaders around the world by providing free, high-quality theological resources. We gladly grant permission for you to print and distribute our courses under these simple guidelines:
No Changes – Course content must not be altered in any way.
No Profit Sales – Printed copies may not be sold for profit.
Free Use for Ministry – Churches, schools, and other training ministries may freely print and distribute copies—even if they charge tuition.
No Unauthorized Translations – Please contact us before translating any course into another language.
All materials remain the copyrighted property of Shepherds Global Classroom. We simply ask that you honor the integrity of the content and mission.