Lesson 6: Wakorintho na Wagalatia: Barua kwa Makanisa Yenye Shida
20 min read
by Randall McElwain
Malengo ya Somo
Kufikia mwisho wa somo hili, mwanafunzi anapaswa: (1) Kujua tarehe na makusudi ya Wakorintho wa 1 na 2 na Wagalatia. (2) Kutoa muhtasari wa dhamira kuu ya Wakorintho wa 1 na 2 na Wagalatia. (3) Kuelewa masuala muhimu ya kutafsiri Wakorintho wa 1. (4) Kujadili mahusiano kati ya mwamini na sheria. (5) Kutambua maana ya kibiblia ya imani kwamba watu wanaokolewa kwa kushika sheria. (6) Kutambua maeneo ya migogoro na mkanganyiko katika kanisa la mwanzo.
(7) Kuhusianisha ujumbe wa vitabu hivi na mahitaji ya dunia ya leo.
► Kariri 1 Wakorintho 1:20-21 and Wagalatia 5:22-23.
Utangulizi
Wasomaji wa kisasa mara kadhaa hudhani kuwa kanisa la kwanza lilikuwa huru mbali na matatizo makubwa. Tunadhani, “Ingekuwa nzuri sana na ajabu kuishi katika kanisa la kwanza ambapo kila kitu kilitendeka katika umoja na kujawa na uamsho” Lakini barua za Paulo kwa Korintho na Galatia zinaonesha picha ya tofauti sana. Makanisa ya karne ya kwanza yalipambana na fundisho la uongo, dhambi kati ya washirika, mkanganyiko kuhusu mafundisho ya muhimu ya Biblia, na maswali kuhusu mamlaka na nidhamu ya kanisa. Kwa maneno mengine, vitabu hivi vinaonesha ulimwengu unaofanana sana na ulimwengu wa leo. Kwa sababu ya hili, barua hizi kwa makanisa yenye shida ya karne ya kwanza zina mengi ya kufundisha makanisa yenye shida ya karne ya 21.
1 Wakorintho
Usuli wa 1 Wakorintho
Mwandishi na Tarehe
Korintho ilikuwa ni bandari iliyoko kwenye sehemu ya ardhi kati ya bahari ya Aegea na Ionia. Shehena ilipakuliwa, kusafirishwa kuvuka ukanda mwembamba wa ardhi, na kupakiwa katika meli zilizokuwa upande mwingine. Eneo la kimkakati la Korintho lilitoa fursa kubwa kwa kusambaa wa injili. Mahali ulipo uliwavuta mabaharia wengi ktuoka dola yote ya Rumi. Hii ilitoa fursa ya kuwahubiria Injili watu kutoka ulimwenguni kote.
Paulo alipanda kanisa Korintho wakati wa safari yake ya pili ya umisheni, mnamo mwaka wa 50 B.K. (Matendo ya Mitume 18:1-18). Pmoja na Akila na Prisila, waamini wawili toka Rumi, Paulo alitumia miezi 18 akihubiri Korintho. Alianza kwa kuhubiri katika sinagogi, Alipotolewa nje ya sinagogi, alihamia kwenye nyumba binafsi iliyokuwa karibu. Wakorintho wengi ikiwepo mtawala wa sinagogi, waliitikia mahubiri ya injili.
Paulo aliandika 1 Wakorintho kuhusu miaka mitano mbele. Barua iliandikwa wakati Paulo akikaa Efeso katika safari yake ya tatu ya umisheni (1 Wakorintho 16:8). Paulo aliandika kwa kujibu matatizo yaliyoibuka katika kanisa la Korintho. Kwa vile asingeweza kusafiri kwa haraka kwenda Korinhto, alituma barua kupitia Timotheo. Timotheo aliteuliwa pia kutoa maelekezo ya ziada wakati wa ziara yake (1 Wakorintho 4:17).
Muundo
1 Wakorintho ni rahisi na vilevile ngumu kutafsiri. Ni rahisi kutafasiri kwa sababu iliandikwa kujibu hali fulani. Katika Warumi, Paulo alielezea masuala magumu ya kimafundisho kwa undani, lakini katika 1 Wakorintho, anashughulikia matatizo moja kwa moja.
Hata hivyo, barua ya aina hii pia yaweza kuwa ngumu kutafasiri kwa sababu hatuna barua kutoka katika kanisa la kikorintho. Lazima tujaribu kutambua matatizo ambayo kwayo Paulo anayajibu kwa kuangalia barua zake. Wakati mwingine, lazima tutofautishe kati ya ushauri wake na nukuu zake kutoka kwa Wakorintho.
Mifano miwili inaonesha jinsi gani Paulo anajibu maswali kutoka Korintho:
1 Wakorintho 7:1 inaanza, “Basi kwa habari ya mambo yale mliyoandika…” Paulo kisha anaandika kifungu ambacho huenda ni nukuu kutoka kwenye barua yao: “ni heri mwanamume asimguse mwanamke.” Paulo kisha anajibu wazo hili (kuwa ni vizuri zaidi kwa wanaume na wanawake kuepuka mahusiano yoyote ya zinaa). Anasema, “Lakini kwa sababu ya zinaa kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe” (1 Wakorintho 7:2).
Vile vile, 1 Wakorintho 8:1 huanza, “Na kwa habari ya vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu…” Anachokisema Paulo baadae ni kama nukuu toka katika barua zao “sisi sote tuna ujuzi.” Paulo anajibu, “…Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga” (1 Wakorintho 8:1).
Kusudi
Barua ya kwanza ya Paulo kwa kanisa la Korintho ilichochewa na ripoti alizopokea kuhusu matatizo haya katika kanisa:
Kulikuwa na matengano.
Uasherati wa waziwazi ulikuwa ukivumiliwa.
Mamlaka ya kitume ya Paulo yalikuwa yakipingwa.
Paulo aliandika 1 Wakorintho kujibu matatizo haya na kujibu maswali ya waamini.
Yaliyomo katika 1 Wakorintho
Katika utangulizi, Paulo anaeleza mamlaka yake kama mtume wa Yesu Kristo na kuwakumbusha waamini wa Korintho kuwa wametakaswa katika Kristo Yesu, na kuitwa kuwa watakatifu (1 Wakorintho 1:1-2). Pia anashughulikia muendelezo wa matatizo yanayoonesha kushindwa kwa wakorintho kuishi kulingana na wito wa Mungu kwa watu wake.
Mgawanyiko (1 Wakorintho 1-4)
Paulo alipanda kanisa Korintho. Mzungumzaji mwenye kipawa Apolo alihubiri baadae baada ya kuelekezwa na Akila na Prisila (Matendo ya Mitume 18:24-28). Yawezekana pia kuwa Petro alitembelea Korintho (1 Wakorintho 9:5). Kanisa lililoko Korintho liligawanyika katika makundi, na kila kundi likidai mmoja wa waalimu hawa kama kiongozi wao. Baadhi walidai kuwa juu ya mgawanyiko, “Mimi ni wa Kristo” (1 Wakorintho 1:12). Hata hivyo, hata kundi hili lilichochewa na roho ya kiburi, na si unyenyekevu. (1 Wakorintho 1:10-12).
Mambo yaliyojadiliwa baadae katika 1 Wakorintho yanaonesha kuwa mgawanyiko huu uliathiri ibada ya wiki na mashangilio ya chakula cha Bwana katika Korintho. Kwa kuongezea, mgawanyiko huu waweza kuwa sababu ya kanisa kutokuwa tayari kushughulikia dhambi kati ya waumini wake.
Paulo anaanza kwa kulinda huduma yake. Wale waliodai kumfuata Apolo walikataa mamlaka ya kitume ya Paulo na kudhihaki muonekano usiopendeza wa Paulo na usemi wake. Paulo anatetea mamlaka yake ya kitume ili kuweka jukwaa la kuhutubia matatizo katika kanisa. Kama baba wa kiroho, Paulo anapenda sana watoto wake (1 Wakorintho 4:14-15) kiasi cha kutowaacha wapotee katika njia zao. Kwa hiyo, Paulo anaanza na ulinzi mkali wa huduma yake: “Paulo, aliyeitwa kuwa mtume wa Yesu Kristo kwa mapenzi ya Mungu…” (1 Wakorintho 1:1).
Tangu baadhi ya waumini watofautishe hotuba rahisi ya Paulo na hotuba ya kuvutia ya Apolo, Paulo anaelezea, “…neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu” (1 Wakorintho 2:4). Paulo hamvamii Apolo[1] lakini anaonesha kuwa huduma yake mwenyewe katika Korintho ilijikita katika nguvu za Roho Mtakatifu akifanyia kazi ujumbe wake. Wakorintho walikuwa wakijisifu kwa hekima ya kibidanamu; Paulo anawaita kurejea katika injili.
Uasherati na Ukosefu wa Maadili (1 Wakorintho 5-6)
► Ni kwa jinsi gani viongozi wa kanisa wangeshuhulikia dhambi waziwazi kati ya waumini?
Kama mji bandari wa Kirumi na mji uliojaa mahekalu ya kipagani yaliyohusisha ukahaba kama sehemu ya ibada zao za sanamu, Korintho ilijulikana kwa upotovu wake wa kizinaa. Neno Corinthianize (“kuwa mkorintho”) lilimaanisha kuharibu maadili ya mtu.
Kanisa la Korintho lilikataa kunidhamisha moja kati ya waumini ambaye alikuwa akiishi katika uhusiano wa kiasherati na mama yake wa kambo, tabia ambayo hukataliwa hata na wapagani (1 Wakorintho 5:1). Kanisa la Korintho lilikuwa na kiburi kiasi cha kukataa kushughulikia tatizo hili.
Maelekezo ya Paulo ni muhimu katika kuelewa nidhamu sahihi ya kanisa. Paulo anataka kuwa wamtenge mkosaji kwa matumaini kuwa atatubu.[2] Kanisa linatakiwa kuhukumu dhambi kati ya waumini wake kwa sababu mbili: kumleta mtenda dhambi katika toba na kuepusha lawama na aibu dhidi ya injili. Paulo hashughulikii matendo ya wasioamini au hata aliyerudi nyuma na kutubu. Anahutubia kwa makusudi dhambi inayoendelea kwa muumini hai wa kanisa.
Kuhusiana na hili, Paulo pia anahutubia kesi za kisheria kati ya waamiini. Wakati Wakorintho wanakataa kuhukumu dhambi wazi katika kanisa, ni wepesi kuchukua malalamiko binafsi kwenda katika mahakama za umma. Paulo anauliza ni kwa jinsi gani wanaweza kuhukumu ulimwengu kama hawana hekima kutosha kuweza kutuliza migogoro kati ya ndugu Wakristo (1 Wakorintho 6:2).
Maswali kutoka kwa Wakorintho (1 Wakorintho 7:1-16:4)
Paulo sasa anahutubia mfululizo wa maswali ambayo Wakorintho waliuliza katika barua waliyomtumia Paulo (1 Wakorintho 7:1). Kila mada inatangulizwa na kifungu, “Basi kwa habari ya…”. Paulo ananukuu swali lao kisha anajibu hoja iliyoibuliwa.
Useja na Ndoa (1 Wakorintho 7:1-24)
Baadhi walifundisha kuwa “…ni heri mwanamume asimguse mwanamke” (1 Wakorintho 7:1). Paulo anajibu kuwa ndoa ni muktadha sahihi wa kujiweka wazi kimapenzi. Katika kipengele hiki, anaelezea pia tatizo la talaka, suala ambalo mahususi kabisa lilikuwa gumu kwa waamini wapya waliokuwa wameoa ama kuolewa na wasioamini.
Wasioolewa na wajane (1 Wakorintho 7:25-40)
Kwa sababu ya dhiki iliyopo, Paulo aliamini kuwa ilikuwa njema zaidi kwa wale ambao hawajaolewa kubaki katika hali ya kutoolewa. Hata hivyo, aliweka wazi kuwa hii ilikuwa ni mtazamo wake binafsi, na sio amri kutoka kwa Bwana. Wakati huo, waamini walikuwa wakiteswa na serikali ya Roma. Paulo angekuwa akiwaza pia kuhusu jinsi gani mateso yangeongezeka kabla ya kurudi kwa Bwana (1 Wakorintho 7:29).
Chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu (1 Wakorintho 8:1-11:1)
►Katika muktadha wa huduma yako, ni mazoea yapi ya kitamaduni ambayo yanaweza kulinganishwa na suala la Wakorintho la chakula lilichotolewa sadaka kwa sanamu?
Mjadala mrefu wa Paulo ni jibu kwa swali gumu la chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu. Wakorintho walikita mjadala wao juu ya ufahamu wao kuwa sanamu sio mungu wa kweli. Paulo anajibu hili kuwa badala ya kukita maamuzi yetu moja kwa moja kwenye ufahamu (ambao huleta kujiinua), tunatakiwa kutenda kwa upendo (ambao hujenga) (1 Wakorintho 8:1).
Paulo anatofautisha kati ya kula katika meza za mahekalu ya kipagani na kufanya manunuzi katika masoko ya umma, Kama mwamini mwenye ufahamu huu anakula katika ukumbi wa karamu katika hekalu, itamjaribu mwamini dhaifu (yule ambaye hana ufahamu huu) kula chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu. Kama mfano wa roho ambayo Wakorintho wanapaswa kuonyesha, Paulo anawakumbusha kuwa alitoa haki yake ya kutegemea msaada wa kifedha kama mchungaji wao ili kutoa injili katika mji wao (1 Wakorintho 9:12, 14-15). Katika namna ile ile, wanatakiwa kuwa tayari kuacha shughuli yeyote inayoweza kusababisha mtu mwingine kutenda dhambi (1 Wakorintho 8:9).
Zaidi, kula katika hekalu la kipagani ilikuwa ni ushirika katika vitendo vya sanamu (1 Wakorintho 10:20).[3] Paulo anahitimisha, “…Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani” (1 Wakorintho 10:21).
Wakati waamini hawatakiwi kula katika hekalu ya kipagani kwa muktadha wa kidini, Paulo anachukulia kitofauti suala la kufanya manunuzi katika soko la umma ambalo huuza nyama tofauti tofauti zilizotolewa sadaka kwa sanamu hapo awali. Kwa sababu hakuna uhusiano wa moja kwa moja na ibada za sanamu, Paulo anasema waamini hawapaswi kuuliza maswali lakini wanapaswa kununua kile kilichopo. Jambo pekee kwa uhuru huu huibuka pale anapokuwepo mtu anayeweza kuchukizwa. Ndugu dhaifu anaweza hata kuhusisha manunuzi ya nyama hii na ibada ya sanamu. Kwa hali hii, Paulo anawakumbusha Wakorintho majukumu ya mkristo kutotaka mema yake tuu bali mema ya nduguye (1 Wakorintho 10:24).
Kanuni kuu ni upendo. Upendo kwa Mungu hunizuia mimi kufanya karamu za sanamu zinazotolewa katika hekalu la kipagani. Upendo kwa ndugu yangu dhaifu hunizuia mimi, kama mwamini imara, kula nyama inayoweza kuharibu imani yake.
Desturi za Ibada na Karama za Kiroho (1 Wakorintho 11:2-14:40)
Paulo baadae anaelezea masuala ya mamlaka, uangalizi wa chakula cha Bwana, na matumizi ya karama za kiroho. Vitendo vya ibada isiyo sahihi vilivyopatikana katika kanisa la Wakoritho ilikuwa ni matokeo ya kiburi na matengano. Wakorintho walitumia karama za kiroho kupandisha hadhi zao wenyewe, badala ya kuhudumiana wao kwa wao kwa hamasa ya upendo.
Ufufuo wa Yesu na wa Wafu (1 Wakorintho 15)
Katika kujibu maswali kuhusu mustakabali wa waamini waliokufa, Paulo anaanza kwa kuthibitisha ukweli wa kihistoria wa ufufuo wa Kristo. Kisha anajadili kuwa ufufuo wa Yesu ni “…limbuko lao waliolala” (1 Wakorintho 15:20). Kwa sababu Kristo aliishinda mauti, waamini wanayo ahadi ya ufufuo.
Kusanyiko la Matakatifu wa Yerusalemu (1 Wakorintho 16:1-4)
Katika safari yake ya tatu ya kimisheni, Paulo alikusanya sadaka kutoka kwa makanisa ya wamataifa ili kuunga mkono waamini walioko Yerusalemu waliokuwa wakipitia mateso. Sadaka hii ilikuwa ya muhimu kwa Paulo kama maelezo ya kivitendo kuhusu fundisho la umoja katika kanisa. Kupitia sadaka hii, waongofu wa mataifa walionesha kuwa ushirika wao katika kanisa ulihusisha jukumu la kushika mkono ndugu zao wa kike na wa kiume (Wayahudi) katika Kristo.
Kuagana (1 Wakorintho 16:5-24)
Paulo anahitimisha barua yake kwa maelezo ya mipango yake ya baadae ya kutembelea Korintho, salamu kwa watu wote, na kwaheri.
[1]1 Wakorintho 16:12 inaonesha kuwa Paulo na Apolo waliungana katika kufanya kazi kwa ajili ya ufalme wa Mungu
[2]“Kumtolea Shetani mtu huyo…” (1 Wakorintho 5:5) pia humaanisha kumtoa kutoka katika kanisa. Nje ya kanisa, yuko katika dunia, ulimwengu wa shetani.
[3]1 Wakorintho 10:1-22 hutumia hadithi ya uaminifu wa wana wa Israeli kama onyo dhidi ya kushiriki ibada za sanamu.
2 Wakorintho
Usuli wa 2 Wakorintho
Muundo
2 Wakorintho iliandikwa mwaka mmoja baada ya 1 Wakorintho. Ilitokea kwamba ziara ya Timotheo haikuleta suluhu kwa matatizo katika Korintho. Kisha Paulo mwenyewe akalitembelea kanisa. Ilikuwa ni ziara ya maumivu, ambayo kwayo kanisa lilikatalia mamlaka yake (2 Wakorintho 2:1). Paulo alirejea Efeso, ambapo hapo aliandika barua nyingine (sasa imepotea) na akaituma kupitia Tito (2 Wakorintho 2:3-9).
Kutoka Efeso, Paulo alisafiri kwenda Makedonia, ambapo alisubiri habari kutoka Korintho. Tito aliripoti kuwa Wakorintho wengi walitubia uasi wao (2 Wakorintho 7:5-16). Hata hivyo, kundi dogo la watu liliendelea kukataa mamlaka ya Paulo, sehemu ya mwisho ya 2 Wakorintho inaelezea kundi hili na kuandaa njia kwa ajili ya ziara ya tatu ya Paulo.
Kusudi
Kusudi la 2 Wakorintho ni:
Kuwasifu Wakorintho kwa kutubu kwao, kama ilivyo ripotiwa na Tito (2 Wakorintho 1-7).
Kukamilisha makusanyo ya sadaka ya Yerusalemu (2 Wakorintho 8-9).
Kuelezea uasi ulioendelezwa na baadhi ya waumini (2 Wakorintho 10-13).
Ratiba ya huduma ya Paulo kwa Wakorintho
Chati ifuatayo inaonesha ratiba ya 1 na 2 Wakorintho. Wakati baadhi ya tarehe hazina hakika, hii ndio ratiba yenye uwezekano mkubwa wa uhusika wa Paulo kwa kanisa la Korintho.
Paulo na kanisa katika Korintho
50 B.K.
Kanisa lilipandwa wakati wa safari ya pili ya kimishenari ya Paulo.
Paulo aliandika barua, ambayo hatuna (1 Wakorintho 5:9).
55 B.K.
Katika Efeso, Paulo aliandika 1 Wakorintho, na Timotheo akapeleka.
Paulo alifanya safari ya “kwa huzuni” kwenda Korintho, wakati ambapo mamlaka yake yalikataliwa (2 Wakorintho 2:1).
Katika Efeso, Paulo aliandika barua ngumu, ambayo hatuna. Alimtuma Tito kuipeleka, na ilisababisha toba (2 Wakorintho 7:8-16).
56 B.K.
Katika Makedonia, Paulo aliandika 2 Wakorintho, na Tito akapeleka.
57 B.K.
Paulo alitembelea Korintho kwa mara ya mwisho (2 Wakorintho 12:14).
2 Wakorintho (inaendelea)
Mada kuu za 2 Wakorintho
Muundo wa 2 Wakorintho unaonesha makusudi mbalimbali. Unatoa mwitikio wa Paulo kwa masuala tofauti tofauti. Mada zinazopatikana katika waraka zinajumuisha:
Utetezi wa Paulo juu ya Utume wake.
Utetezi wa Paulo wa uadilifu wake.
Mipango ya Paulo kwa ajili ya safari ya tatu.
Utetezi wa Paulo juu ya Utume Wake
Kwa aibu ya wazi iliyoonekana, Paulo anatetea utume wake katika kifungu kipana cha maneno. Maadui zake walitumia mateso na udhaifu wa Paulo kama ushahidi dhidi ya mamlaka yake kama mtume. Maadui hawa walijivunia walijitukuza katika mafanikio na nguvu; Paulo alijivunia udhaifu wake, ili kwamba nguvu ya Kristo iweze kukaa juu yake (2 Wakorintho 12:9). Mamlaka yake yanatoka kwa Mungu, ambaye amechagua kutenda kazi kupitia udhaifu wa Paulo kama njia ya kufunua utukufu wa Mungu.
Utetezi wa Paulo kwa Uadilifu wake
Paulo alikusudia kutembelea Korintho mapema lakini alichelewesha ziara yake ili kuruhusu vidonda kutoka katika ziara ya mwanzo kupona. Kwa sababu hii, alisafiri kwenda Makedonia badala ya kwenda moja kwa moja Korintho. Mabadiliko haya ya mpango yalikuwa eneo la Paulo kushambuliwa na adui zake; walimlaumu kwa kutoaminika. Paulo alielezea kwamba alibadilisha mpango wake ili kuhudumia mahitaji yao kwa ufanisi zaidi (2 Wakorintho 1:15-2:4, 12-17).
Mipango ya Paulo kwa ajili ya safari ya tatu
Kuna wale ambao waliendelea kukataa mamlaka ya Paulo na kusema kwamba ni dhaifu. Paulo anaandika kwamba atarudi tena Korintho na kuwaomba watubu kabla ya ujio wake. Mwanzoni mwa barua, anamhakikishia msamaha mkosaji aliyetubu (2 Wakorintho 2:5-11). Mwishoni mwa barua yake, anaomba tena kuhusiana na urejesho. Lengo la Paulo ni upatanisho, na si kisasi.
Wagalatia
Maneno Munhimu
Tunapojiandaa kujifunza kitabu cha Wagalatia, kuna maneno na maana ambazo tunahitaji kuelewa:
Judaizers. Waalimu wa uongo katika kanisa la kwanza ambao walifundisha kwamba tunahesabiwa haki kwa imani katika Kristo pamoja na utii kwa sheria za Kiyahudi. Walikiri kuwa Wakristo, lakini walisisitiza kwamba Waamini wa Mataifa wanapaswa kufuata Sheria ya Kiyahudi ili kuwa sawa mbele za Mungu.
Legalism. Imani kwamba kutimiza matakwa ya sheria ya Musa, au baadhi ya mfumo fulani wa sheria, unamfanya mtu kuwa sawa mbele za Mungu.
Legalist. Mtu ambaye anajaribu kupata wokovu kwa kutii Sheria za Mungu.
Antinomianism. Mafundisho potofu kwamba waamini wako huru kufuata tamaa zao za mwili kwa sababu wamehesabiwa haki kwa imani, si kwa kutii sheria.
Usuli wa Wagalatia
Tarehe
Paulo na Barnaba walihubiri eneo la Kusini la Galatia wakati wa safari yao ya kimisheni ya kwanza, kuanzia 47 B.K. Ni kama Paulo aliandika Wagalatia kati ya 48 B.K kama mwitiko wa shida zilizoibuka kati ya hizi zilibadilika baada ya kuondoka kwake.
Moja ya hoja zinazokubalika zaidi kuhusiana na tarehe hii ni ukweli kwamba Paulo haja taja Baraza la Yerusalemu katika hii barua. Kwa kuwa barua inalenga suala la Mataifa na Sheria (Suala lililoamriwa kwenye Baraza la Yerusalemu mnamo 49 B.K), inaonekana kwamba Paulo angekuwa ametaja baraza hili endapo alikuwa akiandika baada ya kutokea. Tarehe ya 48 B.K. inafanya Wagalatia kuwa waraka wa kwanza wa nyaraka za Paulo.
Kusudi
Baada ya Paulo na Barnaba kuondoka Galatia, Judaizers walianza kuwashawishi waamini wapya hapa. Walimu hawa hawakukataa kwa ujumla kazi ya ukombozi ya Yesu, lakini walihubiri kuwa Mataifa walioamini wanapaswa kutahiriwa na kushika au kufuata sheria za Kiyahudi. Walifundisha kwamba tunahesabiwa haki kwa imani katika Kristo Pamoja na utii kwa sheria.
Kusudi la Paulo la kuandika Wagalatia ni kuwaita kutoka injili ya uongo ya Judaizers na kurudi kwenye injili ya kweli ya wokovu kupitia imani kwa Kristo pekee.
Mada Kuu za Wagalatia
Wagalatia ni waraka wa Paulo wenye maneno magumu sana. Anawakemea Wagalatia kwa ajili ua ujinga wao wa kugeukia injili ya namna nyingine na kuwaita wao warudi kwenye injili ya kweli ya Kristo.
Injili ya Kweli
Tofauti na barua zake za baade, ambapo Paulo mara nyingi anajitambulisha mwenyewe kama Mtume na kama mtumwa wa Yesu Kristo. Katika Wagalatia anajitambulisha mwenyewe kwa maneno yenye mamlaka tu: “Paulo, mtume, (si mtume wa wanadamu, wala kutumwa na mwanadamu, bali na Yesu Kristo, na Mungu Baba aliyemfufua kutoka kwa wafu)” (Wagalatia 1:1). Hii ni lugha ya mamlaka ya kiutume.
Ujumbe wa Paulo ulikuwa ukipingwa na Judaizers katika Galatia. Walikuwa wakisema, “Paulo hakuwa thenashara wa Yesu. Kimsingi, alilitesa kanisa! Kwa nini msikilize ujumbe wake? Yeye sio mtume wa kweli.” Paulo anajibu, “Sikuchaguliwa na mtu au kupitia juhudi za mtu. Mimi ni mtume aliyeitwa na Yesu mwenyewe na Mungu Baba, ambaye alimfufua kutoka wafu.”
Paulo anawataka waamini wa Galatia kujua kuwa injili aliyoihubiri kwao ni injili ya kweli ya Yesu Kristo. Moja ya mahubiri ya Paulo katika mji wa Galatia yamenakiriwa katika Matendo ya Mitume 13:16-41.
► Soma mahubiri ya Paulo katika Matendo ya Matendo ya Mitume 13:16-41. mada gani zimejumuishwa katika mahubiri?
Kuwa makini na yaliyomo katika ufupisho wa injili:
Mungu alitenda kupitia historia ya Israeli ili kumuinua mwokozi (Matendo ya Mitume 13:17-23).
Yesu ni mwokozi, alitangazwa na Yohana Mbatizaji (Matendo ya Mitume 13:24-25).
Yesu alikataliwa na watu wa Yerusalemu pamoja (Matendo ya Mitume 13:27).
Walimsulubisha Yesu, lakini Mungu alimfufua kutoka wafu (Matendo ya Mitume 13:28-30).
Yesu alionekana kwa mashahidi wengi baada ya kufufuka (Matendo ya Mitume 13:31).
Tunahesabiwa haki kwa imani, na sio kwa sheria ya Musa (Matendo ya Mitume 13:38-39). (Huu ulikuwa ujumbe wa muhimu kwa Mataifa walioamini.).
Hii ni injili ya kweli, ujumbe wa kuhesabiwa haki kwa imani pekee. Kwa muda ambao Paulo anaandika Wagalatia, waamini hawa wapya walikuwa wamegeukia injili tofauti, injili ambayo sio hata injili (Wagalatia 1:6-7). Utuwa wa kuhesabiwa haki kwa matendo ya Sheria ni mbali sana na habari njema ya kuhesabiwa haki kwa imani iliyohubiriwa na Paulo.
Mafundisho Kuhusu Kuhesabiwa Haki
Injili ya Kweli
Tunahesabiwa haki kwa imani.
Injili ya Uongo ya Judaizers
Tunahesabiwa haki kwa imani jumlisha kutii sheria.
Injili Potofu Leo
Tunahesabiwa haki jumlisha __________.
Kuhesabiwa haki kwa Neema, na sio Matendo
Paulo alifundisha kwamba tunahesabiwa haki kwa neema, na sio kwa matendo. Katika hoja zake dhidi ya legalism, alionesha mambo manne:
1. Uzoefu wake. Paulo analenga katika injili iliyofunuliwa kwake akiwa njiani kwenda Dameski. Paulo alikuwa adui wa injili, akilitesa kanisa. Alisema “Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu” (Wagalatia 1:14). Kama wokovu ulikuja kwa utii kwa sheria, Paulo hakuhitaji injili, alikuwa mwaminifu kufuata na kutii sheria, lakini Mungu alimfundisha Paulo kwamba, “…hali tukijua ya kuwa mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu…” (Wagalatia 2:16).
2. Uzoefu wa Wagalatia. Wakati ambapo Wagalatia walisikia injili, walipokea Soho kwa imani. Hawakuwa wameokolewa kwa matendo (Wagalatia 3:2). Vile vile haiwezekani kwa wao kuutimiliza wokovu wao kwa utii kwa sheria (Wagalatia 3:3).
3. Uzoefu wa Ibrahimu. “…Ibrahimu alivyomwamini Mungu akahesabiwa haki” (Wagalatia 3:6). Sasa, wale wote wanaoamini ni watoto wa Ibrahimu (Wagalatia 3:7). Kama vile Ibrahimu alihesabiwa haki kwa imani, vivyo hivyo waamini wanahesabiwa haki, si kwa matendo.
4. Sheria yenyewe. Paulo anaonesha kuwa wote wanaotegemea matendo ya sheria wanasimama chini ya “laana ya Mungu, lakini mwenye haki ataishi kwa imani”, lakini “Mwenye haki ataishi kwa imani” (Wagalatia 3:11). Paulo anawatia changamoto waongofu wa Galatia: “Katika ungwana huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa” (Wagalatia 5:1).
Kutimiliza Sheria
► Je, uhuru wetu kutoka matendo ya sheria unaturuhusu sisi kufuata tamaa za dhambi?
Paulo alitambua kwamba ujumbe wa kuhesabiwa haki kwa imani pekee unaweza kutumiwa vibaya.” Msomaji wa barua ya Paulo aliweza amua, “Hizi ni habari za kushangaza! Ninahesabiwa haki kwa neema kupitia imani. Sheria haijalishi. Naweza kufanya chochote ninachotaka kufanya! Naweza kuishi kwa kadri ya tamaa yangu ya mwili.”
Kote katika Warumi na Wagalatia, Paulo anayajibu mafundisho haya potofu. Katika Warumi, anawakumbusha wasomaji wake kwamba wameifia dhambi na kwamba, kwa sababu ya hili, hawawezi kuendelea kuishi tena katika hiyo (Warumi 6:2). Katika Wagalatia, Paulo anawaagiza wasomaji wake: “…lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo. Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako” (Wagalatia 5:13-14).
Uhuru kutoka kwa Sheria sio ruhusa ya kutenda dhambi. Badala yake, tukiwa tumeokolewa kwa neema, roho mtakatifu anatusaidia kumtii Mungu na kutimiza sheria ya upendo.
Paulo hajawahi kufundisha kwamba Sheria ya Mungu haina kazi. Kiukweli, sheria ni ya thamani kwa waamini; kupitia hiyo tunajua jinsi ya kuishi katikactabia inayompendeza Mungu. Lakini tutatii sheria ya upendo, sio utumwa. Upendo unatimiza sheria.
Kuangalia kwa ukaribu Legalism na Utii
Kama mtu akimtii Mungu kwa uangalifu, hiyo ina maanisha yeye ni legalist? Hapana! Mungu anatarajia watoto wake kutii. Legalist ni mtu ambaye anayejaribu kupata wokovu kwa kutii sheria za Mungu. Legalism ni suala la moyo.
Kwa nje, legalist na mtu wa imani wanaweza kuonekana sawa. Lakini legalist anamtii Mungu ili kwamba apate upendeleo wa Mungu, lakini mtu wa imani anamtii Mungu kwa sababu anampenda Mungu na anataka kumpendeza. Hamasisho la mtu utii – sio utii wake wenyewe – ndio kitu ambacho huonesha kama yeye ni legalist.
Mitazamo Mitatu ya Matendo
Legalism
Antinomianism
Upendo wa Mungu
“Nimeokolewa kwa matendo. Ninatii sheria ya Mungu ili kwamba niokolewe.”
“Nimeokolewa kwa neema. Matendo hayajarishi. Ninapaswa kutii sheria ya Mungu.”
“Nimeokolewa kwa neema. Kwa sababu ya upendo wangu kwa Yesu ambaye aliniokoa kwa neema yake, ninamtii Mungu kwa nguvu ya Roho.”
Wagalatia (Mwendelezo)
Mada kuu za Wagalatia (mwendelezo)
Maisha katika Roho
Paulo alilinganisha matendo ya mwili na tunda la Roho (Wagalatia 5:19-23). Kama tunapanda katika mwili, tutavuna uharibifu (Wagalatia 6:8). Kama tunapanda kwa Roho, tutavuna uzima wa milele (Wagalatia 6:8).
Paulo anafundisha kuwa kama tukitembea kwa Roho (kama tunaishi katika utii Kwake) hatutatimiza tamaa za mwili (Wagalatia 5:16). Badala yake, tunda la roho litaonekana katika maisha yetu, na tutatimiliza sheria ya upendo.
Wagalatia 6:1-10 inatuonesha kuwa kuishi kwa sheria ya upendo kuna matokeo muhimu ya kivitendo kwa mwamini:
Tunawarejesha wale walio dondoka katika majaribu.
Tunabebeana mizigo.
Tunafikiri sawasawa kuhusiana na sisi wenyewe.
Tunafanya mema kwa watu wote, hasa waamini wenzetu.
Hii ni uhuru wa kweli wa Kikristo.
Wakorintho na Wagalatia katika Kanisa Leo
Tunapokutana na matatizo katika kanisa, wakati mwingine tunajaribiwa kufikiri, “Haikuwa mbaya hivi wakati wa nyuma!” Hata hivyo Wakorintho na Wagalatia vinatukumbusha kuwa matatizo ya leo siyo mapya. Nyaraka hizi zinaongeza moja kwa moja kwa kanisa la karne ya 21.
1 Wakorintho inatukumbusha kuhusu umoja wa kanisa. Ingawa tunatofautiana katika maeneo mengi, mwili wa Kristo ni mwili mmoja. Ukweli huu unapaswa kutuongoza katika kushughulikia tofauti katika kanisa; unapaswa kutuongoza katika kushughulikia migogoro kati ya waamini, na unapaswa kutuongoza katika kutumia vipawa vyetu kujenga mwili wa Kristo.
Nyaraka hizi pia hutukumbusha kuwa tumeitwa katika huduma ya upatanisho. Katika Wakorintho, Paulo anaonesha kuwa msamaha unapaswa kutolewa bure wakati ambapo kuna mgawanyiko katika kanisa. Vivyo hivyo, katika Wagalatia, Paulo anaonesha kuwa tunapaswa kutafuta kuwarejesha wale waliopotea.
Wagalatia inatukumbusha mafundisho makuu ya kuhesabiwa haki kwa neema kupitia imani. Paulo anaonya dhidi ya bidii yoyote katika kufundisha “Tunahesabiwa haki kwa imani jumlisha chochote kingine.” Hakuna (sio sheria ya Musa, wala matendo wala chochote kingine) inaweza kuongezwa kwa imani katika kazi ya Kristo kama msingi wa kuhesabiwa haki kwetu mbele ya Mungu.
Wagalatia inatukumbusha pia kuhusu matokeo ya maisha ya sheria ya upendo. Sheria ya upendo inabadili maisha yetu kama waamini.
Hitimisho
Mwanzoni mwa 1738, William Holland alishuhudia uhakika wa imani baada ya kusikia kwa Charles Wesley akisoma kutoka maelezo ya Commentary on Galatians ya Martin Luther. Charles Wesley aliandika shajara yake, “Nilitumia masaa baadhi jioni hii kwa faragha pamoja na Martin Luther, ambaye alikuwa baraka sana kwangu... nilifanya kazi kwa bidii, nilisubiri, na kusali ili kuhisi nani aliyenipenda na kujitoa kwa ajli yangu.”
Siku chache tu baadaye, katika Jumapili ya Pentekoste, Charles mwenyewe alishuhudia kuwa na uhakika. Siku nne baadaye, akisikiliza William Holland akisoma kutoka “Preface to Romans,” cha Martine Luther, John Wesley alifikia uhakika wa Imani.
Ujumbe wa kuhesabiwa haki kwa imani ulimbadilisha Luther, Wesleys, na mamilioni ya waamini wengine. Ujumbe huu ni wa muhimu leo kama ilivyokuwa katika karne ya 17.[1]
[1]J. I. Packer, “Introduction,” in Galatians: by Martin Luther, (Wheaton, IL: Crossway Classic Commentaries, 1998), xii.
Somo la 6 Mazoezi
(1) Chagua Mojawapo kati ya mazoezi yafuatayo:
Kama kiongozi cha kujifunzia 1 Wakorintho, andaa muhtasari wa ukurasa mmoja ukionesha kila suala ambalo Paulo analishughulikia katika waraka huu. Muhtasari wako unatakiwa kujumuisha mambo matatu kwa kila suala:
Rejea za vifungu vya maandiko.
Swali au tatizo.
Ufupisho mfupi wa jibu la Paulo.
Andika insha ya ukurasa mmoja juu ya changamoto za wakati huu juu ya fundisho la kuhesabiwa haki kwa imani pekee. Wakati hatupambani na Judaizers na majaribio yao kwa kutaka tohara, ni vitu gani vingine ambavyo huwa vinaongezwa kama msingi wa kuhesabiwa haki?
(2) Mwanzoni mwa somo linalofuata, utafanya jaribio kulingana na somo hili. Soma maswali ya jaribio kwa umakini katika maandalizi.
Somo la 6 Jaribio
(1) Kwa nini Korintho ni mji muhimu sana kwa mkakati wa Paulo wa injili?
(2) Ni nani alifanya kazi pamoja Paulo katika kupanda kanisa Korintho?
(3) Ni matatizo gani matatu makubwa katika kanisa yaliyo muhamasisha Paulo kuandika 1 Wakorintho?
(4) Ni kifungu gani cha maneno kinatoa utangulizi kwa swali ambalo Paulo anajibu katika 1 Wakorintho?
(5) Orodhesha mada kuu tatu zinazo shughulikiwa na Paulo katika 2 Wakorintho.
(6) Nini ni kusudi la Paulo la kuandika Wagalatia?
(7) Judaizers walifundisha nini kuhusiana na namna tunavyohesabiwa haki?
(8) Legalist ni nani?
(9) Ni mambo gani manne ambayo Paulo anayaonesha katika hoja zake dhidi ya legalism?
(10) Kulingana na Paulo, sheria ni ya thamni kiasi gani kwa waamini?
(11) Andika 1 Wakorintho 1:20-21 na Wagalatia 5:22-23 kutoka katika kumbukumbu.
Free to print for ministry use. No changes to content, no profit sales.
SGC exists to equip rising Christian leaders around the world by providing free, high-quality theological resources. We gladly grant permission for you to print and distribute our courses under these simple guidelines:
No Changes – Course content must not be altered in any way.
No Profit Sales – Printed copies may not be sold for profit.
Free Use for Ministry – Churches, schools, and other training ministries may freely print and distribute copies—even if they charge tuition.
No Unauthorized Translations – Please contact us before translating any course into another language.
All materials remain the copyrighted property of Shepherds Global Classroom.