► Soma Zaburi 85 kwa pamoja. Kifungu hiki kinatueleza nini kuhusu Wokovu?
Msalaba
Alama muhimu sana Kikristo ni msalaba. Msalaba huwakilisha tukio ambalo ni kitovu cha historia. Unawakilisha tofauti kati ya Imani ya Kikristo na Imani nyingine.
Msalaba ni siri kwa watu wengi. Hawaelewi kwa nini Yesu alikufa. Hata kama wakisikia kwamba alikufa kwa sababu anatupenda na anataka kutuokoa, hawaelewi kwa nini ilihitajika kutokea. wanajiuliza, “Endapo Mungu alitaka kutusamehe, kwa nini asingefanya tu?”
Kuchanganyikiwa kuhusiana na msalaba kulianza tangu mwanzo kabisa, wakati Wakristo wa kwanza walipoanza kuhubiri Injili. (Soma 1 Wakorintho 1:22-23.) Wayahudi walitarajia kwamba Mungu angejidhihirisha katika nguvu na uweza mkuu mku. Walifikiri kwamba wokovu waliouhitaji ulikuwa ni kuokolewa kutoka katika mateso na ukandamizaji, lakini msalaba ulionekana kuwa ishara ya udhaifu na kushindwa.
Wagiriki/Wayunani walidhani kwamba Mungu angejidhihirisha kwa kutumia hekima. Waliona wokovu waliouhitaji kuwa ni maelezo ya namna ya kuishi maisha bora kikamilifu, lakini kwao msalaba ulionekana kuwa ni upuuzi na kushindwa.
► Kwa nini watu wanachukizwa au wanakwazwa na msalaba?
Msalaba ni kwazo kwa watu wengi. Watu wengi wako tayari kuwa wa kidini. Wako tayari kuamini mambo fulani, kushika desturi za kidini, na kupokea ushauri. Lakini hukasirishwa na wazo kwamba wao ni wenye dhambi kiasi kwamba msalaba ulikuwa ni lazima kwa ajili ya msamaha wao. Wanafikiri kwamba Mungu hapaswi kupinga matendo yao wala tabia yao. Msalaba unawachukiza wengi kwa sababu inamaanisha wao ni wenye dhambi ambao wanahitaji msamaha.
Ili kuelewa kifo ya Yesu cha kujitoa msalabani, ni lazima tuelewe hali ya mwanadamu mwenye dhambi na asili ya Mungu ya utakatifu ambalo ilisababisha njia panda kuu au mtanziko mkuu. Ni lazima tuelewe kwa nini upatanisho ulifanya Mungu aweze kusamehe.
Hali ya Mwanadamu
Kwa sababu ya dhambi ya Adamu, kila mtu anapozaliwa tayari ametengwa na Mungu (Warumi 5:12). Hiyo ina maana kwamba kila mtu ni mbinafsi na huenda njia yake mwenyewe.
Mara tu mtu anapofanya uchaguzi, huanza kutenda dhambi. Kila mwenye dhambi ana hatia ya matendo mengi ya dhambi. (Soma Warumi 3:23.)
Dhambi ni kwenda kinyume na sheria ya Mungu (1 Yohana 3:4; Yakobo 2:10-11). Kwa sababu Mungu ni wa haki kikamilifu, hatoi ahalalishi/hapuuzii dhambi, na kila mtu atahukumiwa kwa kile alichokifanya (2 Wakorintho 5:10; Ufunuo 20:12-13). Hakuna swali kuhusiana na hatia ya mtu au hukumu ambayo anastahili. Kila asiyeamini tayari amekwisha kuhukumiwa (Soma Yohana 3:18-19.)
Mwenye dhambi ambaye hajatubu ni adui wa Mungu (Warumi 5:10). Mwenye dhambi hawezi kuja katika uhusiano hadi hatia zake mbele za Mungu ziwe zimeondolewa.
[1]Mwenye dhambi pia yupo katika hali ya ambayo inamfanya yeye kutokuwa katika hali ya kuwa na mahusiano na Mungu. Mwenye dhambi amepotoka katika nia zake (Waefeso 2:3). Kwa sababu yeye ni mtumwa wa dhambi, mwenye dhambi hana nguvu za kubadilisha hali yake. (Soma Warumi 6:20, Warumi 7:23.)
Kwa hiyo, ni wokovu gani ambao mwenye dhambi anauhitaji? Kwa sababu mwenye dhambi ana hatia, wokovu unamaanisha msamaha. Kwa sababu yeye ni adui wa Mungu, wokovu unamaanisha upatanisho. Kwa sababu yeye ni mpotovu/mwovu, wokovu unamaanisha utakaso. Kwa sababu hana nguvu, wokovu una maanisha ukombozi. Hivi ni vipengere vichache vya wokovu ambavyo mwenye dhambi anavihitaji.
“Ni kwa namna gani mwenye dhambi atahesabiwa haki mbele za Mungu ni swali muhimu kwa kila mwanadamu, kwa sababu hakuwezi kuwa na amani ya kweli au furaha kamilifu wakati sisi ni maadui wa Mungu, ama wakati huu au katika milele.”
- John Wesley, katika mahubiri lenye kichwa cha habari “Kuhesabiwa Haki kwa Imani”
Njia Panda/Mtanziko
Watu wasingeweza kulipia dhambi zao. Sababu moja ni kwamba kila kitu tulichonacho hata hivyo ni mali ya Mungu. Sababu muhimu zaidi ni kwamba dhambi ni kosa dhidi au kinyume cha Mungu asiye na mipaka, na hakuna chochote chenye thamani isiyo na mipaka kinachopatikana kwa ajili ya watu kulipa.
Hakuna chochote kabisa ambacho watu wanaweza kufanya kuhusiana na hitaji lao; hakuna matakwa ambayo yanaweza kuwekwa kwa ajili yao ambayo yanaweza kukamilisha wokovu. (Soma Wagalatia 3:21.) Kama ingekuwa inawezekana kwa watu kukamilisha wokovu wao, kusingekuwa na sababu ya Yesu kufa msalabani. (Soma Wagalatia 2:21.)
► Endapo Mungu alitaka kusamehe, kwa nini asingefanya hivyo tu kirahisi pasipo msalaba?
Kwa sababu Mungu ni mtakatifu na mwenye haki, anapaswa kuhukumu kulingana na kweli na haki (Warumi 2:5-6). Neno upatanisho linarejelea ukweli kwamba dhabihu ya Yesu ni njia ya sisi kupatanishwa na Mungu.
Fikiria kama sadaka au dhabihu ya Kristo isingetokea. Vipi kama Mungu kirahisi tu angesamehe dhambi pasipo upatanisho?
Kama Mungu angesamehe dhambi pasipo upatanisho, ingeonekana kwamba dhambi si muhimu au sio suala kubwa. Ingeonekana kwamba Mungu si mwenye haki, na hata sio mtakatifu. Ingeonekana kwamba machoni pa Mungu kuna tofauti ndogo sana kati ya mtu kufanya kilicho chema na kufanya kilicho kiovu.
Endapo msamaha usingekuwepo bila upatanisho, Mungu asingeabudiwa kama mwenye haki na mtakatifu kwa jinsi alivyo. Msamaha pasipo upatanisho ni dharau kubwa kwa Mungu badala ya kumuheshimu, kwa hivyo hilo lisingefanyika.
Lakini Mungu ni upendo na anataka kusamehe. Hakutaka kuwaacha wanadamu katika hali ya dhambi, apotee milele, hata kama hivyo ndivyo walistahili.
Dhabihu ya Yesu msalabani ilitoa sadaka au dhabihu iliyohitajika yenye thamani isiyo na mipaka. Yesu alikidhi vigezo(1)kwa kuwa asiye na dhambi (mkamilifu na Yeye mwenyewe hakuhitaji wokovu, 2 Wakorintho 5:21), na (2)kwa kuwa Mungu na mwanadamu.
Upatanisho alioutoa ulikwa ndio msingi kwa ajili ya msamaha. Sasa Mungu anaweza kumsamehe mtu ambaye anatubu na kuamini ahadi zake. Hakuna mtu ambaye anaelewa dhabihu ya msalaba na akafikiri kwamba dhambi sio suala kubwa au tatizo zito kwa Mungu.
Upatanisho ulitoa njia ambapo Mungu mwenye haki anaweza kumuhesabia haki mwenye dhambi ambaye anaamihi ahadi zake. (Soma Warumi 3:26.) Warumi 3:20-26 inatoa maelezo ya kimantiki ya namna upatanisho unavyofanya kazi.
Biblia inatuambia kwamba njia ya wokovu ambayo Mungu anatoa ni njia pekee. Endapo mtu atakataa wokovu kwa neema kwa njia ya Imani katika Kristo, hawezi kuokolewa. (Soma Marko 16:15-16; Matendo ya Mitume 4:12; Waebrania 2:3.)
Hii ndio sababu kwa nini ni muhimu kufahamu fundisho la wokovu kwa neema pekee, unaopokelewa kwa Imani pekee. Wokovu ni kwa neema pekee kwa sababu hakuna kitu mtu anaweza kufanya ili kupata au kustahili wokovu. Ni kwa Imani pekee kwa sababu hakuna kitu ambacho tunaweza kufanya kuukamilisha. Tunaweza tu kuamini ahadi za Mungu.
Neema ya Kwanza
► Nani anapiga hatua ya kwanza kuelekea wokovu binafsi, Mungu au mtu mwenyewe?
Mungu ameshachukua hatua ya kwanza kuelekea kumleta mwenye dhambi katika wokovu. Ameonesha utayari wake wa kusamehe kwa kutoa dhabihu ya Yesu msalabani. Sasa neema ya Mungu inafika katika moyo wa mwenye dhambi, ikimuhakikishia yeye kuhusiana na dhambi zake na kumsababisha yeye kutamani msamaha. (Soma Tito 2:11; Yohana 1:9; Warumi 1:20.) Mwenye dhambi asingekuwa na nguvu ya kuacha dhambi zake pasipo msaada wa Mungu (Yohana 6 :44). Mungu anampa mwenye dhambi uwezo wa kuitikia injili. Kama mtu haokolewi, si kwa sababu hana neema, bali kwa sababu hajaitikia neema ambayo Mungu amepatia yeye.
Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi ya ulimwengu wote, na Mungu anataka kila mtu aokolewe. (Soma 2 Petro 3:9; 1 Yohana 2:2; 1 Timotheo 4:10.) Neema ya Mungu inampa kila mtu uwezo wa kuitikia, lakini hamlazimishi mtu yeyote. Hii ndio sababu kwa nini Mungu anamuita mwenye dhambi kuchagua kutubu na kuamini (Marko 1:15).
Toba
► Toba ni nini?
Kutubu ni kugeuka na kwenda uelekeo mwingine. Kitheolojia, inamaanisha kwamba mwenye dhambi anajiona kwamba ana hatia na anastahili hukumu/adhabu, lakini yuko tayari kugeuka kutoka katika dhambi zake.
Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie BWANA, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa (Isaya 55:7).
Toba haimaanishi kwamba mwenye dhambi anapaswa arekebishe maisha yake na kujiweka na kujitengeneza kuwa mwenye haki mbele za Mungu ndipo Mungu amsamehe. Hilo haliwezekani. Lakini mwenye dhambi anapaswa awe tayari kwa Mungu kumuokoa kutoka katika dhambi zake.
► Wokovu unapokelewa kwa neema, sasa kwa nini toba ni muhimu kwa ajili ya wokovu?
Imani ndio hitaji pekee kwa ajili ya msamaha, lakini Imani kwa ajili ya wokovu haiwezi kutokea pasipo toba. Kama mtu hayuko tayari kutubu, basi hayuko tayari kuokolewa kutoka dhambini.
Endapo Mungu atamsamehe mtu ambaye anaendelea kutenda dhambi na anakataa kutubu, hilo halitamletea heshima Yeye kama hakimu mwenye haki wa ulimwengu. Toba ni muhimu, kwa sababu kama mtu hatatubu, maana yake hatambui ubaya wa dhambi. Kama haoni ni kwa nini ageuke kutoka dhambini, basi haoni ni kwa nini anahitaji msamaha.
Endapo mtu hajajiona mwenyewe kama kweli ana hatia, pasipo na udhuru, na anastahili adhabu, bado hajatubu kikweli. Kama anakubali kwamba ni mwenye dhambi lakini anataka kuendelea kutenda dhambi, toba yake haijakamilika, kwa sababu anataka kuendelea kufanya kile ambacho anasema anakikataa.
Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani;ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.(Waefeso 2:8-9).
Anatambua kwamba hakuna chochote anachoweza kufanya (matendo) ambayo yatamfanya yeye kustahili kuokolewa, hata kwa sehemu.
(2) Dhabihu ya Kristo ni toshelevu kwa ajili ya msamaha wake.
Naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote (1 Yohana 2:2).
Kipatanisho inamaana kwamba Yeye amefanya msamaha wetu kuwezekana. Hakuna kingine muhimu kinachoweza kuongezwa katika dhabihu ya Kristo kwa ajili ya msahama wetu.
(3) Yesu alifufuka kutoka kwa wafu, ameshinda dhambi na mauti.
... ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka (Warumi 10:9).
Njia pekee ambayo dhambi na mauti inaweza kushindwa ni kwa Yesu kufufuka. Yesu alifufuka tena kutoka mautini, akitoa ushindi kamilifu juu ya vyote viwili yaani dhambi na mauti.
(4) Mungu amemsamehe kwa sharti la Imani pekee.
Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote (1 Yohana 1:9).
Kama mtu anafikiri kuna masharti mengine kwa ajili ya wokovu, anategemea kuokolewa kwa sehemu kupitia matendo badala ya wokovu kamilifu kwa neema.
Hakikisho
► Ni kwa namna gani watu wanaweza kujua kwa hakika kwamba wameokoka?
Baadhi ya watu wanategemea hisia zao, lakini hisia hubadilika na zinaweza kupotosha.
Biblia inatueleza sisi kwamba tunaweza kufahamu kwamba kwa hakika tumeokoka (1 Yohana 5:13). Tunaweza kuwa na ujasiri kwamba ametukubali. Hatuna haja ya kuishi katika hofu, kwa sababu Roho wa Mungu anatuthibitishia kwamba sisi ni Watoto wa Mungu. Mtume Paulo anasema kwamba Roho Mtakatifu hushuhudia pamoja na roho zetu za kibinadamu kwamba sisi ni watoto wa Mungu (Warumi 8:15-16).
Uthibitisho umekamilika kiasi kwamba hatuwezi kuogopa siku ya hukumu. (Soma 1 Yohana 4:17.) Baadhi ya watu wanatumaini watakubaliwa mbinguni, lakini tunaweza kuwa na uhakika mzuri zaidi ya huo. Haitoshi tu kuamini kwamba wokovu umetolewa kwa wanadamu kwa ujumla; mtu lazima ajue kwamba yeye mwenyewe ameokoka.
Maisha yaliyobadilika ni uthibitisho kwamba mtu ameokoka, lakini uthibitisho huo hautokei mwanzoni mwa maisha ya wokovu. Matokeo ya wokovu hayakuwa na muda wa kutokea. Kwa hivyo, wakati wa toba, maisha yaliyobadilika hayawezi kuwa msingi wa uthibitisho.
Mwamini anaweza kuwa na uhakika wa wokovu wake kwa kufahamu kwamba amefuata njia ya kimaandiko ya wokovu. Kama mtu kweli ametubu na ameamini kama Biblia inavyoelekeza, ana haki ya kuamini kwamba Mungu amemsamehe na amekuwa mtoto wa Mungu.
Endapo mtu anajaribu kufikiri kwamba ameokoka wakati ahajatubu kiukweli, atachanganyikiwa na anajidanganya mwenyewe.
Endapo mtu (1) kweli ametubu, (2) ameamini ahadi za Mungu katika maandiko, na (3) amepokea ushuhuda wa Roho, hatadanganywa. Uthibitisho huu una msingi juu ya neno la Mungu, ambalo ni la kuaminiwa na kutegemewa kweli. Mungu mara zote hushika ahadi zake.
“Imani iokoayo ni imani inayotegemea, kuamini ambako humtegemea Mwokozi kikamailifu.”
—John Stott
Maneno 10 yanayoonesha Vipengere vya Wokovu
Upatanisho: Neno hili linamaanisha kwamba wale ambao mwanzoni walikuwa maadui wa sasa wamepatana. Katika wokovu, Mungu ametupatanisha sisi na tuna amani naye. (Soma 2 Wakorintho 5:19; Warumi 5:1. Mistari hii inazungumza kuhusiana na vyote viwili kuhesabiwa haki na kupatanishwa.)
Ondoleo la Dhambi: Neno hili linamaanisha kwamba rekodi ya dhambi imefutwa. Katika wokovu, rekodi yetu ya dhambi imefutwa. (Soma Waebrania 8:12.)
Kulipa Fidia: Neno hili linarejelea kitu ambacho kilitolewa ili kuondoa hasira au kukidhi hasira ya mtu mwingine. Katika wokovu, sadaka ya Yesu iligeuza hasira ya Mungu ambayo ilikuwa juu/dhidi yetu (Soma 1 Yohana 2:2.)
Wokovu: Neno hili linamaanisha kwamba mtu ameokolewa kutoka katika nguvu za mtu mwingine. Katika wokovu, tumechukuliwa kutoka nguvu za shetani na dhambi. (Soma Luka 1:74; Warumi 6:6, 12-18.)
Ukombozi: Neno hili linamaanisha kwamba gharama ilishalipwa ili kwamba mtu mwingine awe huru. Katika wokovu, kifo cha Yesu ni gharama ili kwamba tuwe huru toka utumwa na adhabu ya dhambi. (Soma Waefeso 1:7; Tito 2:14.)
Kuhesabiwa Haki: Neno hili linamaanisha kwamba mtu ametangazwa mwenye haki, au hana hatia. Katika wokovu, mwenye dhambi mwenye hatia anahesabiwa mwenye haki kwa sababu Yesu aliteseka badala yeke (katika nafasi yake). (Soma Warumi 5:1; 2 Wakorintho 5:19. Mistari hii inazungumza kuhusiana na vyote viwili kuhesabiwa haki na kupatanishwa.)
Utakaso: Neno hili linamaanisha mtu amefanywa mtakatifu. Katika wokovu, mwenye dhambi mwenye hatia anabadilishwa kuwa mtoto mtakatifu wa Mungu. Nyaraka nyingi zinawarejelea waamini kama “watakatifu.” (Soma Waefeso 1:1, Wafilipi 1:1, Wakolosai 1:2.)
Kufanyika Mwana/Kuasiliwa: Neno hili linamaanisha mtu anakuwa mtoto wa mwingine. Katika wokovu, tunakuwa Watoto wa Mungu. (Soma Yohana 1:12; Warumi 8:15.)
Kuzaliwa Upya: Neno hili linamaanisha mtu ameanza maisha tena/mapya. Katika wokovu, mwamini anaanza maisha mapya akiwa na ufufuo wa maisha ya Kiroho ndani yake. (Soma Waefeso 2:1; Yohana 3:3, 5.)
Kugongwa Muhuri: Neno hili linamaanisha kitu fulani kimewekwa alama ili kuonesha nani anakimiliki. Katika wokovu, Roho Mtakatifu ndani yetu anatufanya tuonekane kuwa watu ambao wanamilikiwa na Mungu. (Soma Waefeso 1:13-14.)
Kosa la Kuepuka: Dini Pasipo Toba
Angalizo kwa kiongozi wa darasa: Mshiriki wa darasa anaweza kuelezea sehemu hii.
Kuna aina ya mtu ambaye anaweza kwa urahisi kufikiri kwamba ameokolewa anaposikia kwamba wokovu ni kwa neema kupitia imani. Kiukweli hajatubu kwa sababu hakuona kwamba anahitaji kufanya hivyo. Hakuwahi kujiona kuwa ni mwenye dhambi anayestahili hukumu ya Mungu. Anafikiri kwamba neema inamaanisha kwamba anaweza kwenda katika njia yake mwenyewe. Kwa sababu anakubali kweli ya Ukristo, anafikiri yeye ni Mkristo, ingawaje hana badiliko. Hajawahi kukabidhi mapenzi yake, badala yake, alimkubali Mungu kama sehemu ya maisha yake, na bado kwa sehemu kubwa anaishi kulingana na mapenzi yake. Huu sio mwanzo wa kuwa na uhusiano unaookoa pamoja na Mungu, kulingana na maandiko yanavyoeleza.
► Someni Tamko la Imani kwa pamoja angalau mara mbili.
Tamko la Imani
Maisha, kifo, na ufufuo wa Yesu Kristo umetoa upatanisho kwa ajili ya dhambi ya ulimwengu. Kila mmoja ana hatia ya dhambi na hana nguvu za kujiokoa mwenyewe. Kila mwenye dhambi ambaye anatubu anaweza kupokea neema ya Mungu ya wokovu kwa Imani. Mwamini anasamehewa na anakombolewa kutoka katika nguvu ya dhambi na adhabu. Roho Mtakatifu anabadilisha maisha ya mwamini kutoka kuwa mwenye dhambi aliye na hatia ili kuwa mtakatifu anayemwabudu Mungu. Hakuna njia nyingine ya wokovu. Uumbaji kwa ujumla unaokolewa na hatimaye utarejeshwa na Mungu.
Wokovu Katika Agano la Kale
Angalizo kwa kiongozi wa darasa: Sehemu zote mbili hii na inayofuata ni za hiari. Darasa linaweza kusoma endapo washiriki wanashahuku na mada hii.
Katika Agano la Kale, Mungu alitoa mfumo wa kuabudu kwa sadaka. Sadaka hazikuleta wokovu kwa namna ambavyo kifo cha Yesu kimefanya. Biblia inatueleza kwamba “haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi” (Waebrania 10:4). Kwa hiyo kwa nini sadaka zilitolewa? Zilikuwa ni mfumo wa ibada ambazo ziliwakilisha sadaka ya Kristo ambayo itakuja hapo baadae (mbeleni) (Waebrania 10:1).
Hiyo haikuwa na maana kwamba wokovu haukupatikana hadi nyakati za Agano Jipya. Mtume Paulo alipokuwa akielezea fundisho la kuhesabiwa haki kwa neema kupitia Imani, alitoa mifano ya Abraham una Daudi kuonesha kwamba halikuwa wazo au fundisho jipya (Warumi 4:1-8). Yesu alisema kwamba Nikodemu alipaswa kuwa tayari amefahamu kuhusiana na kuzaliwa upya kwa sababu yeye alikuwa mwalimu wa Agano la Kale (Yohana 3:10). Paulo alimwambia Timotheo kwamba Maandiko Agano la Kale yangemfanya yeye mwenye hekima kuhusiana na wokovu (2 Timotheo 3:15). Kwa hivyo, injili ilikuwepo wakati wa Agano la Kale ingawaje haikuwa imeelezewa katika maneno ya wazi kama katika Agano Jipya.
Kulikuwepo na baadhi katika Agano la Kale ambao walielewa neema. Hawakufahamu taarifa za kina kuhusiana na upatanisho, au namna gani unafanya kazi, lakini walielewa kwamba Mungu aliweka msingi kwa ajili ya msamaha. Dhabihu zilikuwa ni mfumo wa kuielezea Imani hiyo, kama ambavyo tuna mfumo na namna ya kuabudu leo (kwa mfano, chakula/meza ya Bwana). Dhabihu zingekuwa hazina maana endapo zingetolewa pasipo Imani na utii, kama ambavyo mifumo na namna za ibada hazitakuwa na maana endapo hazitafanyika kwa moyo na maisha ambayo yametolewa kwa Mungu. Zaburi 51 na Isaya 1:11-18 inaonesha kuwa toba na Imani vilikuwa muhimu sana katika nyakati za Agano la Kale.
Zaburi 85, ambayo iliandikwa miaka mingi kabla ya upatanisho wa Kristo kutokea, kwa uzuri inaelezea neema ya Mungu na namna ambayo Mungu husamehe dhambi. Inazungumzia kuhusiana na hasira iliyomalizwa. Zaburi 85:10 inasema, “Fadhili na kweli zimekutana, Haki na amani zimehusiana.” Hii ni picha ya ajabu ya wokovu kupitia upatanisho. Pasipo upatanisho, huruma za Mungu zingekuwa na mipaka na ukweli kwamba sisi ni wenye hatia. Haki ya Mungu ingetufanya sisi kuwa maadui badala ya kuruhusu amani. Katika upatanisho, haki inatimizwa, na rehema zinaoneshwa.
Wokovu wa Uumbaji Wote
Maneno kuokolewa au wokovu yanatumika kwa kiasi kikubwa katika Biblia. Yanarejelea zaidi ya wokovu binafsi, ambao umeelezewa katika somo hili. Maneno haya yanarejelea kwa kile ambacho kimefanyika awali (Waefeso 2:8), kile kinachotokea sasa (1 Wakorintho 1:18), na kile kitakachotokea baadae (Marko 13:13). Dhana hii inarejelea kile kilichotokea kwa watu (ambacho kimekuwa kinasisitizwa katika somo hili) lakini pia kinarejelea makundi ya watu, kama vile Wayahudi (Warumi 1:16), Wamataifa (Warumi 11:11), Nyumba yote (Luka 19:9), au familia (Waebrania 11:7), au inaweza kurejelea mtu kuokolewa kutoka katika hatari ya kimwili (Mathayo 14:30).
Wanadamu wa kwanza walipofanya dhambi, laana ilikuja juu ya uumbaji wote (Mwanzo 3:17). Wokovu utakapokamilika, uumbaji utarejeshwa pia.
Wokovu huanza na urejesho wa Kiroho. Waamini wanaokolewa kutoka dhambini, na wanaishi katika baraka za Mungu. Hata hivyo, hawajapata uzoefu wa kuokolewa kutoka katika vipengere au Nyanja za kimwili za laana ya dhambi. Bado wana miili ambayo inazeeka na kufa.
Asili au uumbaji bado upo katika laana ya dhambi. Hatujauona ulimwengu katika namna ambayo Mungu aliiumba hapo Mwanzo. Tunaona asili kwamba imejaa viumbe hatarishi na viumbe wako katika mgogoro baina yao. Katika ulimwengu wetu, viumbe wengi wanakufa kwa ajili ya wengine kuishi.
Wakati unakuja ambapo viumbe wote wanarejeshwa au kufanywa upya (Ufunuo 21:1; Waebrania 1:10-12). Warumi 8:18-25 inaelezea tumaini la Wakristo kwa ajili ya ulimwengu kuwekwa huru dhidi ya laana ya dhambi.
Somo la 8 Mazoezi
(1) Zoezi la Kifungu: Kila mwanafunzi atapewa mojawapo ya vifungu vilivyoorodheshwa hapa chini. Kabla ya kipindi kinachofuata cha darasa, unapaswa kusoma kifungu na kuandika aya kuhusiana na somo la somo hili.
Zaburi 51
Isaya 1:11-18
Warumi 3:20-26
Warumi 8:19-25
Waefeso 2:1-10
(2) Jaribio: Utaanza kipindi kijacho cha darasa kwa jaribio juu la Somo 8. Jifunze kwa umakini maswali wakati wa maandalizi.
(3) Zoezi la Kufundisha: Kumbuka kupanga na kuripoti muda wako wa kufundisha nje ya darasa.
Somo la 8 Jaribio
(1) Kwa nini msalaba unawachukiza wengi?
(2) Orodhesha mambo manne ambayo ni kweli kuhusiana na mwenye dhambi ambaye hajatubu.
(3) Kwa nini msamaha wa dhambi pasipo upatanisho ni dharau au kutomuheshimu Mungu?
(4) Ni kwa njia gani mbili ambazo Yesu kwa kipekee alikidhi vigezo vya kuwa dhabihu?
(5) Ni nini unapaswa kuwa mtazamo wa mwenye dhambi ambaye hajatubu?
(6) Kama mtu ana imani iokoayo, anaamini nini?
(7) Ni kwa namna gani watu wanaweza kujua kwa hakika kwamba wameokoka?
Free to print for ministry use. No changes to content, no profit sales.
SGC exists to equip rising Christian leaders around the world by providing free, high-quality theological resources. We gladly grant permission for you to print and distribute our courses under these simple guidelines:
No Changes – Course content must not be altered in any way.
No Profit Sales – Printed copies may not be sold for profit.
Free Use for Ministry – Churches, schools, and other training ministries may freely print and distribute copies—even if they charge tuition.
No Unauthorized Translations – Please contact us before translating any course into another language.
All materials remain the copyrighted property of Shepherds Global Classroom.