Kwa nini uhamasisho wa maandiko unamaanisha kuwa maandiko hayana makosa.
Maneno iliyohamasishwa, isiyoweza kuwa na makosa, na isiyokuwa na makosa.
Kwa nini Biblia imekamilika na haiwezi kuongezewa habari za ziada.
Jinsi Biblia ilivyo chanzo kikuu na mamlaka ya mwisho ya kanuni.
Jinsi Biblia ilivyo muhimu katika maisha ya kila siku ya Mkristo.
Kauli ya kanuni za Kikristo kuhusu Biblia.
(2) Mwanafunzi ataepuka kusikiliza mamlaka yasiyofaa au kujifunza Biblia akiwa na kusudi finyu.
Utangulizi
Kidokezo kwa kiongozi wa darasa: Kwa kawaida kipindi kitaanza na mtihani juu ya somo la awali na mapitio ya malengo ya somo la awali. Kwa kuwa hili ni somo la kwanza, nenda kwenye maandiko yaliyo hapa chini.
► Someni Zaburi 119:1-16 pamoja. Kifungu hiki kinatuambia nini kuhusu Biblia?
Mungu, Muumba wa ulimwengu, amenena. Amejifunua mwenyewe na kusudi la uumbaji wake. Ukweli ambao Mungu ametufunulia unaitwa ufunuo. Kuna kitabu katika Biblia kinachoitwa “Ufunuo,” lakini neno ufunuo linaweza pia kutumika kwa ajili ya ukweli wote ambao Mungu amefunua.
► Je, baadhi ya njia ambazo Mungu ametumia kutufunulia ukweli ni zipi?
Aina Mbalimbali za Ufunuo
Kwa sababu Mungu amefunua ukweli kwa njia tofauti, tunazungumza kuhusu aina mbili: Ufunuo wa Jumla na Ufunuo Maalum.
Ufunuo wa Jumla
Ufunuo wa Jumla ni kile ambacho Mungu ametuonyesha kuhusu yeye mwenyewe kupitia uumbaji wake. Tunaona akili na uwezo wa ajabu wa Mungu katika muundo wa ulimwengu.
Uumbaji wa juu zaidi wa Mungu ni mwanadamu. Tunajifunza mambo fulani kumhusu Mungu tunapotazama jinsi watu wameumbwa. Ukweli kwamba tunaweza kufikiri, kuvutiwa na umaridadi, na kutofautisha mema na mabaya (ingawa si kwa njia kamili) unatuonyesha kwamba ni lazima Muumba wetu ana uwezo huo kwa kiwango cha juu zaidi. Tunajua kwamba Mungu lazima awe mtu anayeweza kufikiri na kuwasiliana kwa sababu sisi tuna uwezo huo.
Kwa sababu Ufunuo wa Jumla unatuonyesha kwamba Mungu anaweza kunena, tunatambua kwamba Ufunuo Maalum unaweza kutokea. Kwa sababu Mungu anaweza kunena, inawezekana kwamba kuna jumbe kutoka kwa Mungu na hata kitabu kutoka kwa Mungu.
Kupitia Ufunuo wa Jumla, watu wanajua kwamba kuna Mungu, kwamba wanapaswa kumtii, na kwamba tayari wamemwasi. (Soma Warumi 1:20-21.) Lakini Ufunuo wa Jumla hautuelezi jinsi ya kuingia katika uhusiano sahihi na Mungu. Ufunuo wa Jumla unatuonyesha umuhimu wa Ufunuo Maalum kwa sababu unaonyesha kwamba watu ni wenye dhambi na hawana kisingizio mbele za Muumba wao, lakini hautuambii suluhu.
Mungu alitupa Ufunuo Maalum kupitia maandiko yaliyohamasishwa na kupitia Yesu, Mwana wake. Ufunuo Maalum unaeleza hali ambayo Ufunuo wa Jumla unaonyesha kuwa ndio hali yetu: tumeanguka na tuna hatia. Ufunuo Maalum unaeleza Mungu, unaeleza Anguko na dhambi, na unaonyesha njia ya kupatanishwa na Mungu.
Fikiria kama hungejua kwamba kuna Biblia. Unatambua kwamba kuna Mungu. Unajua
kwamba kuna tatizo kati yako na Mungu. Hujui ni nini kitatokea baada ya kifo. Hujui kusudi la maisha. Hujui jinsi ya kumkaribia Mungu.
Kisha fikiria kwamba mtu fulani anakuonyesha kitabu na anakuambia kwamba kimetoka kwa Mungu ili kujibu maswali hayo. Je, unaweza kufikiria jinsi kitabu hicho kingekuwa cha thamani?
“Siamini kwamba mtu yeyote anaweza kuhubiri Injili bila kuhubiri Sheria. Ukishusha Sheria utakuwa unafifisha nuru ambayo kwayo mwanadamu anaona hatia yake.”
Charles Spurgeon
Dai la Biblia
► Biblia inadai nini kujihusu? Toa mifano kadhaa ya kauli za Biblia zinazoonyesha kwamba inadai kuwa imetoka kwa Mungu.
Hebu tuzungumze kuhusu dai ambalo Biblia inatoa kujihusu. Kisha, tutaangazia ushahidi kwamba Biblia ni kweli. Biblia inadai kuwa Neno la Mungu. Katika Agano la Kale, kuna kauli zaidi ya 3,000 kwamba jumbe zilitoka kwa Mungu, ambazo mara nyingi husema tu, “Bwana alisema….”[1] Yesu alichukulia kuwa Agano la Kale lilihamasishwa na Mungu. (Soma Mathayo 5:17-18; Yohana 10:35; Marko 12:36.) Waandishi wa Agano Jipya walichukulia kuwa Agano la Kale limetoka kwa Mungu. (Soma Matendo 3:18; 2 Timotheo 3:16; 2 Petro 1:20-21.) Waandishi wa Agano Jipya walichukulia kwamba maandishi ya Agano Jipya yalihamasishwa na Mungu. (Soma 1 Wakorintho 14:37; 2 Petro 3:16.)
Ikiwa mtu hakubali dai la Biblia kujihusu, anapaswa kuangalia ushahidi. Hebu fikiria tena kwamba hujui kuhusu Biblia. Unajua kwamba Mungu ni mtu na anaweza kunena akitaka. Kwa hivyo, unajua kwamba kitabu kinaweza kutoka kwa Mungu. Kisha mtu anakuonyesha kitabu na anakuambia kwamba ni kitabu kutoka kwa Mungu.
► Unawezaje kujua kwamba Biblia kwa kweli ni Neno la Mungu? Ungetarajia iweje?
Mahali ambapo injili inahubiriwa, popote duniani, watu huhisi usadikisho wa ndani wa ukweli wake. Wanapoamini injili na kutubu, wanapata msamaha wa Mungu na maisha yaliyobadilika. Kwa watu wengi, hiyo ndio sababu yao ya kwanza ya kuamini Biblia (Soma 1 Wathesalonike 1:5.)[2]
Kisha kwa wale walio na uhusiano na Mungu, Roho wa Mungu hunena kupitia maandiko, akiwapa ufahamu na usadikisho. Jinsi Roho Mtakatifu anavyoitumia Biblia inathibitisha kwamba ni Neno la Mungu. (Soma Waefeso 6:17.)
Tunapotembea katika uhusiano na Mungu, tunapata kwamba Biblia hufunua kwa usahihi asili yake na jinsi anavyofanya kazi nasi. Biblia inatuonyesha njia ya
kuanza uhusiano na Mungu na njia ya kuendelea kutembea pamoja naye. Huu ni ushahidi kwamba Biblia ni Neno la Mungu. (Soma Zaburi 119:1-2.)
Lakini je, ukitaka ushahidi usiyotegemea matukio ya kiroho uliopitia wewe mwenyewe? Watu katika dini nyingine pia hupitia matukio ya kiroho, lakini matukio hayo hayatokani na ukweli. Je, tunawezaje kujua kwamba matukio ya kiroho tunayopitia yanatokana na ukweli?
► Je, kuna ushahidi kwamba Biblia ni sahihi katika mambo inayosema?
Biblia iliandikwa na waandishi zaidi ya 40 katika kipindi cha miaka 1,500. Wengi wa waandishi hao hawakufahamiana. Kwa kawaida tungetarajia nini kutoka kwa kitabu kama hicho? Tungedhani kwamba itakuwa na kila aina ya makosa na makinzano. Lakini fikiria mambo yafuatayo kuhusu Biblia. Maelfu ya maeneo ya kijiografia yaliyotajwa katika Biblia yamepatikana; maelfu ya matukio ya kihistoria yamethibitishwa kuwa yalitokea na watu binafsi wanaotajwa katika Biblia wamethibitishwa kuwa walikuwepo katika historia; hakuna kitu chochote kilichogunduliwa kimekanusha taarifa ya Biblia; na Biblia haijikanushi yenyewe kamwe. Kauli kama hizi si kweli kuhusu kitabu chochote kingine kilichowahi kuandikwa. Ushahidi unaunga mkono dai la Biblia kwamba ilihamasishwa na Mungu.
Tukitumia vipengele sita, tunaweza kueleza kwa ufupi ushahidi unaounga mkono dai la Biblia kuwa ni Neno la Mungu. Tunajua Biblia kweli ni Neno la Mungu kwa sababu:
► Je, tunamaanisha nini kwamba Biblia imehamasishwa?
Uhamasisho ni kazi isiyo ya kawaida ambayo kupitia kwayo Mungu alijifunua na kuleta ufunuo huo kwa njia ya maandishi. Biblia ndio matokeo ya mwisho ya uhamasisho huo. Biblia imehamasishwa tofauti na vitabu vingine vyote. Uhamasisho wa Biblia unamaanisha kwamba ni Neno la Mungu kikamilifu, hata maneno yenyewe yaliyotumiwa.
Wakati mwingine watu huhisi kana kwamba wamehamasishwa wanapokuwa na mawazo makuu, lakini Biblia inamaanisha zaidi ya hilo inapodai kuwa imehamasishwa na Mungu.
Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki (2 Timotheo 3:16).
Ingawa maandiko yalitiririka kutoka kwenye kalamu zilizokuwa mikononi mwa wanadamu, msisitizo wa kifungu hiki ni kwamba Biblia ilitoka kwa Mungu. Kwa sababu Biblia imetoka kwa Mungu, inaweza kutegemewa kwa ajili ya kufundisha kanuni. Ni bora kuliko kile kilicho bora zaidi ambacho watu wanaweza kufanya.
Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu (2 Petro 1:20-21).
Vifungu hivi katika 2 Petro vinasema kwamba waandishi waliongozwa na Roho Mtakatifu. Usahihi wa waandishi wa Biblia haukutegemea ufahamu wao wenyewe. Ukweli kwamba walihamasishwa au kuongozwa na Roho Mtakatifu katika uandishi wao unaonyesha kwamba kutegemeka kwa maandishi yao hatimaye kulitegemea Mungu. Biblia inategemeka kama vile Mungu.
Uhamasisho Ulikuwaje?
► Je, baadhi ya njia ambazo waandishi wa Biblia walipokea ukweli wa Mungu kabla ya kuandika zilikuwa zipi?
Wakati mwingine watu hujiuliza jinsi uhamasisho ulifanya kazi. Mungu aliwasilishaje ukweli wake na kuhakikisha kwamba umeandikwa kwa usahihi? Ukweli wa kwanza tunaopaswa kutambua kuhusu mtindo wa Mungu wa ufunuo ni kwamba ni wa aina mbalimbali. Hatumii njia moja tu. (Soma Waebrania 1:1.)
Wakati mwingine Mungu alizungumza kwa sauti ya kusikika, kama vile alipozungumza na Musa (Kutoka 33:11). Wakati mwingine alitoa ndoto au maono, na mwandishi akayaeleza.[1] Labda sehemu ya maandiko iliyokuja moja kwa moja zaidi kutoka kwa Mungu na kuandikwa ilikuwa agano kati ya Mungu na Israeli ambalo liliandikwa kwa kidole cha Mungu (Kumbukumbu la Torati 9:10). Sehemu nyingine za maandiko zinaonekana kuwa zilisemwa na zikaandikwa, kwa sababu vifungu vikuu katika Kutoka, Mambo ya Walawi, na Hesabu vinakuja baada ya kauli inayosema, “Bwana akanena na Musa, akisema…”
Uhamasisho haumaanishi kwamba Mungu alimnenea mwandishi maneno kwa sauti ya kusikika. Tunaona tofauti za haiba na mitindo ya uandishi kati ya waandishi mbalimbali. Kwa mfano, mtindo wa Paulo ni tofauti sana na wa Petro. Mtazamo wetu wa uhamasisho unatambua jinsi Mungu alivyotumia haiba, misamiati, mitindo ya uandishi, elimu na utafiti wa kihistoria wa wanadamu.
Mtazamo sahihi wa uhamasisho ni kwamba Mungu alimhamasisha mtu mzima, akitumia fikira na haiba ya mwandishi mwanadamu kueleza ukweli wa kiungu, si tu kufunua ukweli bali pia alisimamia mchakato wa kuandika ili maandiko yawe na usahihi kamili.
Watu wengine hufikiri kwamba Mungu alitoa tu mawazo ambayo alitaka kuwasilisha na mwandishi mwanadamu aliyaeleza vizuri kadiri anavyoweza, na kufanya makosa yasioepukika na ya kibinadamu katika maelezo yake. Mtazamo huo hauambatani na maelezo ya Biblia kuhusu uhamasisho. Biblia inaeleza kwamba waandishi waliongozwa na Roho Mtakatifu katika uandishi wao, kwa hivyo tunajua kwamba hawakuachwa waandike peke yao, wakifanya makosa.
Kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu, haisemi jambo lolote lisilo sahihi kwa sababu Mungu hakosei (Soma Mithali 30:5.) Kwa kuwa Mungu alijifunua katika historia iliyorekodiwa katika Biblia, ni lazima maelezo yote yawe sahihi ili tuwe na ufunuo wa Mungu unaotegemeka. Kwa hivyo, kwa sababu ya maelezo ya Biblia kuhusu uhamasisho, tunajua kwamba Mungu aliongoza uandishi ili maandiko yawe sahihi kikamilifu.
[1]Kwa mifano ya ufunuo kupitia maono, tazama Danieli 7 na 8, na sehemu kubwa ya kitabu cha Ufunuo.
Maneno Yanayotumiwa Kutetea Usahihi Kamili wa Biblia
Iliyohamasishwa
Biblia ilihamasishwa, kumaanisha kwamba ni Neno la Mungu kikamilifu, hata maneno yenyewe yaliyotumiwa. Neno hili awali lilitosha kuthibitisha kutegemeka na usahihi kamili wa Biblia, lakini sasa baadhi ya watu wanaosema wanaamini kwamba Biblia ilihamasishwa wanakataa kwamba ni sahihi kikamilifu. Maneno yafuatayo yameanza kutumika kutetea vipengele muhimu vya uhamasisho.
Isiyoweza kuwa na makosa
Neno hili linamaanisha “haiwezi kushindwa.” Tunaposema kwamba Biblia haiwezi kuwa na makosa, tunamaanisha kwamba inaweza kuaminiwa na kamwe haiwezi kutupotosha. Biblia haiwezi kuwa na makosa si tu katika maelezo yake ya kikanuni, bali pia katika kila kauli inayotoa.
Isiyokuwa na makosa
Neno hili linamaanisha “bila makosa.” Biblia ni sahihi katika kila kauli inayotoa. Kwa kuwa Mungu hawezi kamwe kusema uongo au kufanya kosa (soma Tito 1:2) na Biblia ni Neno la Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Biblia haina makosa. Mtu akisema kwamba Biblia inaweza kuwa na makosa kwa sababu wanadamu walihusika katika uandishi wake, anasahau maelezo kuhusu uhamasisho katika 2 Petro 1:21: waandishi waliongozwa na Roho Mtakatifu. Mtazamo wa kibiblia na wa kihistoria kuhusu uhamasisho ni kwamba
Biblia nzima imehamasishwa, hata maneno yake yenyewe, na kwa hivyo haina makosa. (Soma Mathayo 5:18.)
Je kuhusu Makosa katika Kunakili?
Kabla ya uchapishaji wa mashine kuwepo, hati zote pamoja na maandiko zilinakiliwa kwa mkono. Hatuna hati za asili zilizoandikwa na Paulo, Isaya au Musa. Miongoni mwa maelfu ya nakala za kale zilizoandikwa kwa mkono tulizo nazo katika lugha ya Kigiriki na Kiebrania, kuna tofauti ndogo ndogo, na hatuwezi kujua katika hali zote ni maneno gani hasa yalitumiwa katika maandishi ya asili. Hata hivyo, tofauti hizo ni ndogo sana kiasi kwamba hakuna kanuni inayoweza kutiliwa shaka kwa sababu ya maneno hayo. Kwa sababu tunajua kwamba nakala za asili hazikuwa na makosa, na kwa sababu tofauti katika nakala hizo ni ndogo sana, tunajua kwamba tunaweza kuamini kila kauli inayotolewa na Biblia.
► Tunajuaje kwamba Biblia ni sahihi ingawa ilinakiliwa kwa mkono mara nyingi?
► Ni sababu gani mbalimbali zinazofanya watu wengine wafikiri kwamba Biblia ina makosa?
Kwa Nini Watu Wengine Wanafikiri Biblia Ina Makosa?
Wakati mwingine watu wengine hudai kwamba Biblia ina makosa. Hiyo ni kwa sababu hawaelewi asili ya Biblia.
Biblia ilitumia mawasiliano ya kawaida ya wanadamu. Kwa mfano, kuna kifungu kinachosema jua linasonga angani. Wanasayansi wengi wanaamini kwamba dunia inazunguka, badala ya jua kusonga, lakini pia wanasema jua huchomoza na kutua. Waandishi wa Biblia walieleza tu kama walivyoona.
Pia kuna kauli za kishairi, kama “Milima iliruka kama kondoo waume” (Zaburi 114:4), au “miti yote ya kondeni itapiga makofi” (Isaya 55:12). Huo ni mtindo wa fasihi ambao ni dhahiri haumaanishi moja kwa moja kile kinachosemwa.
Wakati mwingine waandishi walinukuu watu wengine, wakiwemo watu ambao hawakuongozwa na Roho. (Kwa mfano, hotuba za marafiki wa Ayubu zimeandikwa, ingawa Mungu alisema yale waliyosema hayakuwa sahihi (Ayubu 42:7).)
Hakuna lolote kati ya hayo ambalo ni tatizo kwa kanuni ya uhamasisho. Mungu aliongoza mchakato wa kuandika ili kuhakikisha kwamba hatimaye kile kitakachoandikwa kitakuwa Neno lake.
Wakati mwingine watu hufikiri wanaona mkinzano katika Biblia, lakini wanahitaji kuiangalia kwa makini zaidi. Kwa mfano, Marko 5:1-2 na Luka 8:26-27 inatuambia kuhusu mtu
aliyekuwa amepagawa na pepo ambaye aliwekwa huru na Yesu. Mathayo 8:28 inatuambia kwamba kulikuwa na watu wawili waliokuwa wamepagawa na pepo waliowekwa huru. Huo si mkinzano. Luka na Marko hawakusema kulikuwa na mtu mmoja tu. Walichagua kumwangazia mtu mmoja ambaye alikuwa na historia katika eneo hilo. Mtu akiona kauli za Biblia ambazo zinaonekana kukinzana, hapaswi kuwa na haraka ya kufikia hitimisho fulani, bali achukue muda wa kuelewa muktadha.
Biblia kwa ajili ya Mkristo
► Je, baadhi ya njia ambazo Mkristo anapaswa kutumia Biblia ni zipi?
[1]Biblia inatoa sheria ya Mungu. Kufuata sheria hakutuokoi, lakini sheria inatuonyesha jinsi Mungu anavyotaka tuishi. Sheria ya Mungu inaonyesha asili ya Mungu. Tunapaswa kuifuata kwa sababu tunataka kuwa kama Mungu. Kwa sababu tunampenda Mungu, tunapaswa kuipenda sheria yake. Zaburi 119 inaeleza jinsi mtu anayemwabudu Mungu anavyopaswa kufurahia sheria ya Mungu. Mtu anayempenda Mungu atamwomba Mungu aubadili moyo wake ili ufanane na mapenzi ya Mungu. Haiwezekani mtu anayempenda Mungu kutojali kuhusu kumpendeza Mungu.
Neno la Mungu ni nuru. Mtume Petro anatuambia kwamba ulimwengu uko katika giza la kiroho, na Neno la Mungu ni nuru ya kutuongoza katika njia tunayopaswa kufuata. (Soma 2 Petro 1:19-21; tazama pia Zaburi 119:105.) Mtu hapaswi kamwe kufuata mawazo au hisia zinazokinzana na Neno la Mungu. Roho Mtakatifu hawezi kamwe kumwongoza mtu kufanya jambo ambalo Biblia inasema si sahihi.
Neno la Mungu ni chakula chetu cha kiroho. Hamu ya kula ni ishara ya afya bora, na Mkristo atatamani Neno la Mungu kama mtoto mchanga anavyotamani maziwa (1 Petro 2:2). Kadiri Mkristo anavyokomaa, ataweza kuelewa kwa kina zaidi ukweli wa Mungu, kama vile mtoto anavyojifunza kula chakula kigumu (1 Wakorintho 3:2). Ni lazima Mkristo ajilishe kiroho kila siku kwa kula Neno la Mungu.
Biblia ni ngao yetu dhidi ya Shetani. Tumeagizwa kujivika silaha za kiroho. Upanga ambao Roho Mtakatifu anatupatia ni Neno la Mungu (Waefeso 6:17). Yesu alijibu majaribu ya ibilisi kwa kutumia maandiko (Mathayo 4:3-4).
Neno la Mungu ni ukweli unaohitaji mwitikio wetu. Yesu alilinganisha neno na mbegu zilizopandwa (Luka 8:11-15). Baadhi ya mbegu hazikufanya vizuri kwa sababu ardhi haikuwa imetayarishwa. Tunaposoma Biblia, ni lazima tuitikie ukweli wake na kusali ili Mungu alete matunda katika maisha yetu kupitia Neno lake.
“Uongo mkubwa zaidi ambao utamaduni wetu unaamini leo ni kwamba sisi ni watu wazuri na kwamba, kwa sababu Mungu ni mwenye upendo, hataadhibu dhambi.”
Francis Chan
Kwa sababu Biblia Ni Neno la Mungu…
Kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu…
Kamwe haitapitwa na wakati au ikose kuwa na umuhimu. Ni muhimu kwa watu wote, mahali popote na wakati wote.
Ni mwongozo wa kupambanua mapenzi ya Mungu, kwa kuwa Mungu hawezi kamwe kujipinga au kubadili mawazo yake.
Ni mwongozo wetu wa kupata yaliyo bora zaidi maishani, kwa kuwa Mungu, Muumba wetu, aliitoa kama maagizo kwa ajili yetu.
Ina kila kitu tunachohitaji kujua ili kuokolewa na kutembea katika uhusiano na Mungu.
Ingawa tunajifunza kutoka kwa wachungaji na kutoka kwa desturi za kanisa, hakuna wazo linaloweza kukubalika ambalo linakinzana na maandiko kwa sababu maandiko ndio mamlaka ya mwisho.
Roho Mtakatifu hutufunulia Neno la Mungu ili tulielewe na hutuelekeza kulitii.
► Mungu bado ananena, lakini je, tunapaswa kutarajia kwamba kuna kitu kinachoweza kuongezwa kwenye Biblia?
Je, Biblia Imekamilika?
Tangu mtume wa mwisho afe, kanisa limechukulia Biblia kuwa kitabu kilichokamilika. Kanisa halikuchagua tu maandishi fulani ili kuyaita maandiko; badala yake, lilitambua kwamba maandishi fulani yalihamasishwa na Mungu na yalikuwa na mamlaka ya kimaandiko. Maandishi ambayo yalitambuliwa kuwa maandiko yalitimiza sifa ambazo hakuna maandishi mengine ya baadaye yangeweza kutimiza.
Kwa vitabu vya Agano la Kale, kanisa lilihifadhi maandishi ambayo Israeli ilikuwa imehifadhi kama maandiko. Hatimaye, vitabu vya Agano Jipya vilitambuliwa kama maandiko kwa msingi wa sifa zifuatazo:
Uhusiano wa kihistoria na mitume
Uwezo wa kujithibitisha vyenyewe
Kukubalika na kanisa lote
Matumizi ya heshima ya Agano la Kale
Manufaa katika kupinga mafundisho potovu
Mungu bado ananena, lakini je, kuna kitu kinachoweza kuongezwa kwenye Biblia sasa? Haiwezekani kwamba maandishi yoyote mapya yanaweza kutimiza sifa husika ili kujumuishwa katika maandiko ya asili. Kwa mfano, hakuna maandishi mapya yanayoweza kuhusishwa na mitume, kwa kuwa hawako tena pamoja nasi. Pia, hakuna maandishi yoyote mapya yanayoweza kukubaliwa na kanisa zima kote ulimwenguni.
Maandiko ni kamili na yanatosha kwa ajili ya wokovu na kuishi maisha ya Kikristo (2 Timotheo 3:14-17). Hakuna kitu chochote muhimu kinachoweza kuongezwa katika maandiko kwa sababu tayari yana kila kitu tunachohitaji. Watu wanaodai kuwa wanapokea ufunuo mpya badala yake wanapaswa kutumia muda wao kusoma ufunuo ambao Mungu ametoa tayari. Watapata hapo kila kitu wanachohitaji na watalindwa kutokana na kufanya makosa.
Makosa ya Kuepuka
Kidokezo kwa kiongozi wa darasa: Washiriki wawili wa darasa wanaweza kueleza sehemu hii na sehemu inayofuata.
Kudhoofisha Mamlaka ya Biblia
Mamlaka yako ya mwisho ni yapi? Wakristo wengi wangesema kwamba Biblia ndio mamlaka yao, lakini kwa kweli wanaamini zaidi hisia zao wenyewe. Mtu atasema kitendo fulani ni sawa kwa sababu hahisi ana hatia anapokifanya. Mtu huyo anafanya hisia zake kuwa mamlaka ya mwisho badala ya Biblia.
Kuna sababu nyingi kwa nini watu wanaweza kutoichukulia Biblia kwa uzito. Labda mtu fulani wanayemheshimu anapuuza fundisho lililo wazi la Biblia, na hilo linawatia moyo kufanya vivyo hivyo. Labda wana hatia ya kufanya jambo ambalo Biblia inakataza, na wanajaribu kutafuta njia ya kutetea matendo yao wenyewe. Labda hawajui yale ambayo Biblia inafundisha. Ni lazima tufanye kila juhudi kuielewa Biblia na kutii mamlaka yake.
Kujifunza Biblia Ukiwa na Kusudi Finyu
Biblia ndio chanzo kikuu cha kanuni za Kikristo. Ni mamlaka ya mwisho kwa swali lolote la kikanuni. Hata hivyo, ni tatizo watu wanapojifunza Biblia ili tu kupata uthibitisho wa kanuni zao. Hawatumii Biblia kama chakula cha kiroho. Wanafikiria tu jinsi ya kuonyesha kwamba mtu mwingine amepotoka. Ni sawa kwetu kuendeleza na kutetea kanuni zetu tukitumia maandiko. Hata hivyo, ikiwa hiyo ndio njia yetu ya pekee ya kutumia Biblia, tutapoteza furaha inayotokana na kuitumia katika uhusiano wetu wa kibinafsi na Mungu.
Watu wengine husoma Biblia kwa kusudi la kuhisi kutiwa moyo tu. Tunapaswa kukumbuka kwamba makusudi ya Biblia yanajumuisha kufundisha, kusadikisha watu juu ya makosa yao na kuwarekebisha (2 Timotheo 3:16). Hatupaswi kuruka amri za Biblia, tukitafuta ahadi zinazotufanya tujihisi vizuri zaidi. Labda Mungu anataka kusadikisha juu ya makosa yetu au kuturekebisha leo au kutufundisha jambo fulani.
Makosa ya Madhehebu Potovu
Makundi fulani ya kidini yanadai kuamini Biblia, lakini yanafanya kitu kingine kiwe mamlaka yao ya mwisho. Wanadai kwamba ni wao tu ndio wanaoweza kueleza Biblia, wakitumia ufunuo au mfumo fulani maalum ambao ni wao tu ndio walio nao. Kanuni zao muhimu zaidi haziwezi kuthibitishwa kupitia Biblia.
Huenda wakawa na kitabu kingine wanachotumia kama maandiko pamoja na Biblia. Huenda wakasema kwamba Biblia haitegemeki kwa sababu ina makosa ya utafsiri na unakili.
Mawazo hayo yanadokeza kwamba Biblia si kamili kama Neno la Mungu. Kwa watu hao, kitu kingine kinakuwa mamlaka ya mwisho.
► Someni kauli ya imani pamoja angalau mara mbili.
Kauli ya Imani
Biblia ni Neno la Mungu. Mungu aliwahamasisha waandishi ili waandike bila kufanya makosa. Biblia inajumuisha kila kitu tunachohitaji kujua ili kuokolewa kutokana na dhambi na kutembea katika uhusiano na Mungu. Biblia ndio chanzo kikuu cha kanuni zetu na ndio mamlaka ya mwisho. Mkristo anapaswa kujifunza Biblia kila siku ili kumjua Mungu vizuri zaidi, kuongozwa na Mungu, kulishwa kiroho na kuishi maisha yenye maana na yenye furaha.
Mazoezi ya Somo la 1
(1) Zoezi la Kifungu cha Biblia: Kila mwanafunzi atapewa mojawapo ya vifungu vilivyoorodheshwa hapa chini. Kabla ya kipindi kinachofuata cha darasa, unapaswa kusoma kifungu chako na kuandika aya moja kuhusu kile ambacho kifungu hicho kinasema kuhusu mada ya somo hili.
Zaburi 119:33-40
Zaburi 119:129-136
Mithali 30:5-6
Mathayo 5:17-19
2 Timotheo 3:15-17
2 Petro 3:15-16
Ufunuo 22:18-19
(2) Mtihani: Utaanza darasa linalofuata kwa kufanya mtihani juu ya Somo
la 1. Jiandae kwa kuchunguza maswali ya mtihani kwa makini.
(3) Zoezi la Kufundisha: Angalau mara tatu wakati wa kozi hii, utawafundisha watu wasioshiriki katika darasa lako somo moja au sehemu ya somo. Mafundisho haya yanaweza kufanywa katika darasa kanisani, kikundi cha kujifunza Biblia nyumbani, mkusanyiko wa familia au mazingira mengine. Unawajibika katika kuunda fursa hizi na kutoa ripoti kwa kiongozi wa darasa lako.
(4) Kumbuka siku zote kusoma somo linalofuata ili ujiandae kwa darasa linalofuata.
Mtihani wa Somo la 1
(1) Ufunuo wa Jumla Ni Nini?
(2) Je, Mungu ametoa Ufunuo Maalum kwa njia gani mbili?
(3) Je, Ufunuo Maalum hufanya mambo gani matatu yasiyofanywa na Ufunuo wa Jumla?
(4) Je, Biblia inatoa dai gani kujihusu?
(5) Orodhesha sababu sita zinazotufanya tujue kwamba Biblia ni Neno la Mungu.
(6) Je, kwa nini Biblia ni yenye faida kwa mafundisho, kwa kuwaonya watu makosa yao, kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki? (2 Timotheo 3:16).
(7) Je, Bibilia inatoa maelezo gani juu ya uhamasisho yanayotuhakikishia kwamba waandishi walizuiwa ili wasifanye makosa?
(8) Orodhesha njia nne za uhamasisho ambazo Mungu alitumia.
(9) Je, inamaanisha nini kwamba Biblia ilihamasishwa?
(10) Je, inamaanisha nini kwamba Biblia haiwezi kuwa na makosa?
(11) Je, inamaanisha nini kwamba Biblia haina makosa?
SGC exists to equip rising Christian leaders around the world by providing free, high-quality theological resources. We gladly grant permission for you to print and distribute our courses under these simple guidelines:
No Changes – Course content must not be altered in any way.
No Profit Sales – Printed copies may not be sold for profit.
Free Use for Ministry – Churches, schools, and other training ministries may freely print and distribute copies—even if they charge tuition.
No Unauthorized Translations – Please contact us before translating any course into another language.
All materials remain the copyrighted property of Shepherds Global Classroom. We simply ask that you honor the integrity of the content and mission.