Mafundisho Na Mazoezi Ya Kanisa
Mafundisho Na Mazoezi Ya Kanisa
Audio Course Purchase

Search Course

Type at least 3 characters to search

Search through all lessons and sections in this course

Searching...

No results found

No matches for ""

Try different keywords or check your spelling

results found

Lesson 8: Msaada wa Kanisa la Mahali

13 min read

by Stephen Gibson


Maagizo ya Yesu

► Mwanafunzi atapaswa kusoma Luka 10:1-9 kwa ajili ya kikundi. Je, kuna kitu gani kisichokuwa cha kawaida kuhusiana na maelekezo ya Yesu aliyowapa wanafunzi wake wakati alipowatuma kwenda kufanya huduma?

Wanafunzi walitumwa kuwa wa kwanza kuhubiri injili katika maeneo mengi ya vijiji. Yesu alikuwa na uwezo wote na nyenzo zote na alikuwa na uwezo wa kuwapa kitu chochote. Angeweza kuwapa fedha za kuwatosha katika kununua chochote ambacho wangehitaji katika kukidhi mahitaji ya watu wengine. Angeweza kuwapa nguvu za kujigawia mkate na Samaki wao wenyewe na kwa ajili ya watu waliokuwa wanawahubiria. Wangeweza kugawa chakula kwenye kila Kijiji walichokuwa wanakitembelea.

Badala yake, aliwatuma bila fedha. Aliwaambia wategemee kupata misaada yao kutoka kwa watu waliokuweko katika vijiji walivyotembelea. Mitume walikwenda kama Yesu alivyowaagiza, na walipatiwa mahitaji yao (Luka 22:35).

► Je, kwa nini Yesu aliwatuma kwa njia hii?

Huduma yao iliwavutia watu sahihi. Kwa kuwa walihubiri injili kwanza, waliwavutia watu waliokuwa wanahitaji injili. Kwa kuwa walikuwa na mahitaji, waliwavutia watu waliotaka kusaidia. Walikuwa na watu wazuri sana kwa ajili ya mwanzo wa kanisa.

Je, ingekuwaje kama wangeenda kwenye vijiji wakiwa na kila kitu ambacho walikuwa wanakihitaji pamoja na vitu vya kuwapa watu? Wangewavutia watu ambao siyo sahihi. Wangeweza kukusanya kundi la watu ambao wangekuja kwa ajili tu ya kupata kitu chochote. Baada ya hapo, huduma ingekuwa endelevu tu kwa kuendelea kuwapa vitu. Hawangeweza kupata wa kuwasaidia bila kuwalipa kwanza. Hawangeweza kuwa na kikundi cha watu ambao wangekuwa ni chanzo kizuri cha wao kuweza kuanzisha kanisa.

Mfumo ambao Yesu alikuwa amewapa uliweza kuanzisha kikundi ambacho kingefanyika ni kanisa. Lilikuwa ni kundi la watu walisisimka na ujumbe wa injili na kutamani kusaidia. Ni muhimu sana kwamba makanisa yaweze kuanza katika njia iliyo sahihi.

Sababu Zinazofanya kanisa liweze Kupata msaada wa Mahali Pale Pale

► Je, ni kwanini kanisa lipate msaada wa mahali pale pale? Kabla ya kuangalia orodha ya sababu zinazofuata hapa chini, ni sababu gani nyingine unazoweza kuzifikiria?

1. Yesu alituonyesha kwamba huduma ya mahali inapaswa ianze kwa njia iliyo sahihi. Aliwatuma wanafunzi wake kutoka nje bila ya kuwa na fedha ili kwamba huduma yao iweze kuwa kivutio kwa watu waliokuwa wanavutiwa na injili na ambao walikuwa wanataka kutoa msaada.

2. Mungu alitoa maelekezo ya kutoa kwa ajili ya makanisa ya Agano Jipya. Makanisa yalitakiwa kutuma misaada ya uwezeshaji kwa ajili ya kanisa la kwanza katika Yerusalemu (1 Wakorintho 16:1-3; 2 Wakorintho 8:1-7, 2 Wakorintho 9:1-6). Yalitakiwa kuwatunza wajane na watu wengine waliokuwa wahitaji katika kanisa (1 Timotheo 5:16; Yakobo 1:27, Yakobo 2:15-16). Yalitakiwa kutoa msaada kwa watu walioko kwenye huduma za kudumu (Wagalatia 6:6).

3. Mungu huliwezesha kila kanisa kuwa mwili wa Kristo pale mahali lilipo (1 Wakorintho 12:27). Hii inamaanisha kwamba kanisa lililokuwa linaweza kufanya maamuzi na kuendeleza maono kwa ajili ya huduma zake lenyewe. Hali hyo haiwezi kutokea kama kanisa ni tegemezi kwa viongozi wake wa nje kwa ajili ya msaada na mwelekeo wa kanisa. Msaada wa kifedha kutoka mahali pale lilipo ni muhimu sana kwa ajili ya kukua kwa kanisa.

4. Mungu hubariki mapato ya kifedha ya watu wanaotoa zaka. Laana iko juu ya mapato ya kifedha ya watu ambao hawatoi zaka (Malaki 3:8-10).

5. Kuwa tegemezi kwa misaada kutoka nje kunaliweka kanisa la mahali/mtaa katika hatari. Uchumi wa Kitaifa na wa Kimataifa hazina uhakika. Endapo wafadhili wa nje wataacha kutoa misaada yao, makanisa yaliyo tegemezi kwao yatataabika.

6. Wachungaji wanapaswa wahudumiwe na watu wao wanaowahudumia (Wagalatia 6:6). Kusanyiko la kanisa la mtaa linatambua kama mchungaji wao ni mwaminifu. Wanajua kama anautumia muda wake mwingi kwenye huduma. Hapaswi kupewa misaada ya muda mrefu na watu walio mbali na kanisa.

► Je, kuna matatizo gani yanayojitokeza kutokana na kuwa tegemezi kwa misaada ya mbali?

Sera za Kifedha za Umisheni kulingana na Utawala wa Ndani wa Kanisa la mahali

Umisheni wa Kimataifa au dhehebu unapaswa kufuata baadhi ya kanuni ambazo kwa njia nyingine zinasaidia makanisa. Shirika linapaswa liwe makini katika kusaidia kwa njia ambayo itayafanya makanisa yawe imara zaidi, kuliko kuyafanya yawe tegemezi zaidi. Hapa kuna mifano ambayo umisheni au dhehebu wanaweza wakaikuza.

1. Kusisitiza kuhusu kutoa zaka kama msingi wa mapato ya kifedha wa Mkristo. Kama kusanyiko la kanisa litakuwa halitoi zaka, Mungu hataweza kubariki mapato ya kifedha ya kanisa. Kama tayari hawafanyi kile ambacho walitakiwa wakifanye, itakuwa wana uelewa potofu kuhusiana na huduma ya mapato ya kifedha. Msaada wa nje unafanya mambo kuwa mabaya zaidi badala ya kuwa mazuri zaidi.

2. Fanya miradi ambayo itatoa kitu cha kudumu kuliko msaada kuwa mapato ya kila siku, Shirika linapaswa litumie fedha kwa ajili ya miradi ambayo itaweza kusaidia kanisa liwe na nguvu zaidi kifedha, kuliko kutoa mishahara ambayo inafanya kanisa liwe tegemezi kwa misaada kutoka nje. Mahali ambapo mishahara ya kila mwezi kutoka katika shirika tayari inakuwa ipo, shirika linapaswa lifanye mpito wa kulisaidia kanisa liweze kujitegemea lenyewe.

3. Usianzishe huduma ambazo kamwe haziwezi kupata msaada wa mahali pale pale ulipo. Mashirika hayapaswi kuanzisha mambo ambayo yatakuwa tegemezi kutoka misaada ya nje kwa muda wote itakapokuwa inafanya kazi. Lengo ni kuanzisha huduma au shughuli za biashara ambazo zinaweza zikawa ni za kanisa la mahali na ziendeshwe kutokea mahali pale pale. Kwa mfano, uwepo wa shule unapaswa uwe ni huduma ya kanisa la mahali.

Juhudi zozote za huduma ambazo kamwe hazina uwezekano wa kufadhiliwa na watu wa mahali pale pale zinatakiwa ziwe ni kitu cha muda ambacho kinalenga kukamilisha kusudi fulani kwa haraka bila ya kutengeneza utegemezi (Mifano: Ufanyaji wa makongamano na uendeshaji wa semina mbalimbali).

4. Kuujengea uwezo uongozi wa kanisa la mahali kuliko kulipita kando. Wakati watu wa nje au viongozi wa ngazi za juu wanapotoa misaada moja kwa moja kwa watu wenye mahitaji bila ya kupitia kwa viongozi wa kanisa la mahali wale walioko kwenye huduma za kanisa la mahali wanaonekana kwamba hawana ufanisi wowote. Kuliko kutoa misaada moja kwa moja kwa watu wenye kuhitaji misaada katika kanisa la mahali, shirika linapaswa liwawezeshe viongozi wake katika kukidhi mahitaji hayo.

► Je, kuna mifano gani iliyopo ya aina potofu ya misaada ya umisheni? Je, kuna mifano gani iliyo sahihi ya aina ya misaada ya umisheni?

Kuepuka huduma ya misaada

Kanisa halipaswi kuweka kando vipaumbele vyake kwa ajili ya “huduma ya msaada.” Kuna watu na mashirika ambayo yanataka kutoa rasilimali zao kwa ajili ya kuondoa umaskini lakini hawana mawasiliano ya moja kwa moja na watu ambao ni wahitaji. “Mashirika ya misaada” ni mashirika ambayo hukusanya rasilimali kutoka kwa wafadhili kwa ajili ya kuwapa watu wenye uhitaji wa kupewa misaada. Wakati mwingine wakuu wa misaada hiyo hupata mishahara kutokana na rasilimali walizo nazo. Wakati mwingine kunakuwepo na udanganyifu, wafadhili pamoja na walio na uhitaji wa kupewa misaada wanatapeliwa. Hata wakati ambapo misaada inaenda kwa watu sahihi, watu wanaotoa huduma ya msaada wanakuwa na mwenendo wa kutaka kumfurahisha zaidi mfadhili kuliko kujaribu kuelewa mahitaji halisi ya watu.

Huduma ya msaada kwa kawaida hulipita kando kanisa la mahali. Inatolewa katika njia ambayo inapuuzia uhusiano wa kanisa na watu wanaopokea msaada. Kutoa kuna matokeo mazuri wakati inapofanyika kupitia kwa kanisa, kwa viongozi ambao wanajua hali halisi za watu, na kwa njia ambayo inaonyesha umuhimu wa kanisa.

Endapo shirika litakuwa linatimiza mahitaji ya watu maskini (kama chakula) bila ya kubadilisha hali zao, inamfanya yule maskini kuwa tegemezi zaidi. Kama watakuwa wanazo rasilimali za kutosha, wanaweza wakaanzisha jumuiya za watu ambao ni tegemezi. Wakifanya hivyo kuendelea kufanya hivi kwa kipindi kirefu, watakuwa wanainua vizazi vipya vyenye watu ambao ni tegemezi.

Umisheni haupaswi kuwepo kwenye sehemu ya huduma ya msaada na ukasahau vipaumbele vya kanisa. Kwa kufanya hivyo hatimaye kwa pamoja kutaliumiza kanisa na watu wenye mahitaji.

► Je, ni mifano gani ambayo ulishawahi kuiona ya huduma ya msaada na matokeo yake?

Mpango wa Mungu katika Kuwawezesha Wachungaji

► Mwanafunzi atapaswa kusoma Kumbukumbu la Torati 18:1-5 kwa ajili ya kikundi. Je, kifungu hiki kinatuelezea nini kuhusiana na msaada wa kifedha kwa ajili ya huduma?

Kuwasaidia kifedha watu walioko kwenye huduma ya wakati wote ilikuwa mpango wa Mungu tangu nyakati za Agano la Kale. Makuhani walipaswa kuungwa mkono kwa kazi yao hekaluni. Hawakupokea urithi wa ardhi, kwa sababu hawakutakiwa kuwa na shughuli za kilimo.

Uwezeshwaji wa kifedha kwa ajili ya watu walioko kwenye huduma ya wakati wote ulikuwa ni mpango wa Mungu tangu wakati wa Agano la Kale. Makuhani au makasisi walikuwa wawezeshwe kwa ajili ya kazi zao katika hekalu. Hawakupewa kumiliki sehemu yeyote ya kipande cha ardhi, kwa sababu hawakutakiwa kujishughulisha sana katika mambo ya kilimo.

Wakati mwingine Israeli iliposhuka katika kiwango chao cha uaminifu wa kuabudu, uwezeshwaji kwa ajili ya makuhani au makasisi pia ulishuka. Ilikuwa ni ishara ya kukosa uaminifu wakati watendakazi katika hekalu wanapoliacha hekalu na kuondoka kwenda kutafuta njia nyingine za kujisaidia wenyewe (Nehemiah 13:10).

► Mwanafunzi atapaswa kusoma 1 Wakorintho 9:1-14 kwa ajili ya kikundi. Je, kifungu hiki kinatuelezea nini kuhusiana na msaada wa kifedha kwa ajili ya huduma?

Paulo alisema kwamba mpango wa Mungu ni kwa ajili wahubiri wa injili kuwezeshwa na huduma zao, kama ilivyo katika mfumo wa Agano la Kale (1 Wakorintho 9:13-14). Paulo alitumia vielelezo kadhaa kuhusiana na kanuni hii. Mkulima anawezeshwa na mazao anayolima. Mchungaji wa wanyama anawezeshwa kutokana na ongezeko la mifugo yake. Askari haendi vitani kwa gharama zake mwenyewe.

Mtume anasema kwamba huduma inahitaji uangalizi kamili wa mchungaji. Hali iliyo nzuri ni kwa yeye kuweza kuachana na shughuli nyingine za ajira (aya ya 6). Mtume anasema kwamba huduma pia ni lazima iweze kumwezesha mke wa mchungaji, ikimaanisha pia ni pamoja na watoto (aya ya 5).

► Mwanafunzi atapaswa kusoma 1 Timotheo 5:17-18 kwa ajili ya kikundi. Je, kifungu hiki kinatuelezea nini kuhusiana na msaada wa kifedha kwa ajili ya huduma?

Wazee watawalao vema wanatakiwa wahesabiwe kustahili heshima maradufu. Aya ya 18 inaonyesha kwamba heshima hiyo ni uwezeshwaji wa kifedha.

► Mwanafunzi atapaswa kusoma Wagalatia 6:6 kwa ajili ya kikundi.

Mtu anayepokea mafao kutoka katika huduma anatakiwa atoe msaada katika kuwezesha huduma.

Mwanzo wa kawaida wa Kuanza Kanisa

Tangu wakati wa karne ya kwanza ya kanisa, makanisa mengi yamekuwa yakianza kama vikundi vidogo vilivyokusanyika nyumbani kwa watu. Majengo ya makanisa hayakuwahi kuwepo kwa miaka mia mbili ya kwanza, lakini bado Ukristo ulienea kwa haraka sana. Katika majiji makubwa, maelfu ya watu walikutanika kwenye ibada za makanisa, lakini bado walikuwa wanakutana tena kwa vikundi majumbani kwa watu.

[1]Paulo alipokuwa akisafiri na kufanya uinjilisti, kipaumbele chake kilikuwa ni kuanzisha kanisa katika kila eneo alilokuwa akipita. Njia hiyo pamoja na mambo mengine ilihusisha kuteua wachungaji (Matendo 14:23; Tito 1:5). Mchungaji katika kila eneo alikuwa ni mtu ambaye tayari alikuwa anaishi katika eneo hilo na alikuwa sehemu ya ushirika husika.

Mchungaji kwa kawaida huanzisha huduma yake bila ya kuwa na msaada wa kifedha. Anakuwa anamsaidia mmishenari au anaanza kuhubiri injili bila ya uwepo wa mmishenari kwa sababu ana matamanio ya kutoa msaada. Ataanza kuonyesha karama na uwezo kwa ajili ya huduma. Atafanya hayo siyo kwa ajili ya kulipwa, bali kwa sababu ya ari ya kiroho.

Kikundi cha watu walioamini kinapokuwa kimeundwa, majukumu ya mchungaji huongezeka na kutumia muda mwingi zaidi. Kikundi kinapaswa kiwe msaada wa kumwezesha mchungaji ili aweze kutumia muda wake mwingi vizuri kwenye huduma. Mwanzoni uwezeshaji unaweza usiwe katika hali ya ukamilifu, lakini unaweza ukawa unaongezeka polepole.

► Je, utasemaje kwa mtu ambaye anasema kwamba anataka kuwa mchungaji lakini anangojea msaada wa kifedha?


[1]

“Tusisifu wale wapangaji wasio na makazi ambao huzurura huku na kule bila kuungana na kanisa lolote, kwa sababu popote pale hawaoni maadili yao yakitimia, daima kuna kitu kinachokosekana.”

– Philip Melanchthon, Loci

Mambo yenye upekee

Paulo alielezea kwamba Mpango wa Mungu ni kwa ajili ya wachungaji kupata uwezeshwaji. Hata hivyo, huduma yake mwenyewe wa wakati mwingine ilikuwa ya kipekee. Kwenye maeneo kadhaa alifanya kazi kwa ajili ya kujisaidia yeye mwenyewe (1 Wathesalonike 2:9; 2 Wathesalonike 3:8).

Kanisa Jipya haliwezi kuwa na uwezo wa kumtegemeza mchungaji kwa ukamilifu wote. Wakati mmishenari anapoondoka na kwenda kwenye eneo jipya kwa ajili ya kuhubiri injili, inawezekana kusiwepo na msaada wa kumtosha. Kwa hiyo, mhubiri anapaswa awe ni mtu ambaye anahubiri kwa sababu ana matamanio ya kufuata wito wa Mungu. Atafanya huduma kwa sababu iko kwenye moyo wake, hata kama halipwi chochote.

Kama mchungaji hayuko tayari kwa hiari yake kufanya shughuli zitakazosaidia yeye mwenyewe na kuhubiri bila ya malipo wakati inapobidi, hana upendo kwa Mungu ambao ingepaswa awe nao. Watu wengine watafanya kwa sababu ya fedha na hawatafanya kwa ajili ya Mungu. Tunapaswa kwa hiari yetu wenyewe kufanya kila kitu kwa ajili ya Mungu. Kama mchungaji atafikiri kwamba yeye ni muhimu sana katika kufanya kazi au shughuli za kujisaidia mwenyewe, anapaswa akumbuke mfano wa Paulo. Kamwe haijawahi kutokea kuwepo na mmishenari maarufu kuliko Paulo, lakini alikuwa na hiari ya kufanya chochote kile kilichokuwa muhimu kwa ajili ya kukamilisha huduma.

Paulo alisema kwamba alihubiri injili kwa sababu ya wito wa Mungu. Alihubiri kwa sababu hakuna namna nyingine ambayo angeweza kumfurahisha Mungu vinginevyo. Mhubiri analo jukumu maalumu, na atahukumiwa na Mungu kama hatatii (1 Wakorintho 9:16-17).

► Je, ni kitu gani kinatakiwa kiwe ni motisha kwa mchungaji kwa ajili ya huduma yake?

Mtume Petro alisema kwamba mzee wa kanisa ni mchungaji ambaye anapaswa kulichunga kundi la Mungu, na awe mwenye kutaka sana kulisimamia na kulichunga. Lengo lake halipaswi liwe katika kutaka fedha (1 Petro 5:1-2).

Dema alikuwa mtu aliyekuwa akimsaidia Mtume Paulo, lakini baadaye aliachana naye kwa sababu ya kupenda mambo ya ulimwengu huu (2 Timotheo 4:10). Jaribu kufikiria heshima aliyokuwa ameipata Dema kwa kufanya kazi na Paulo kwenye kizazi cha kwanza cha kanisa, lakini bado aliachana na huduma kwa sababu ya kutaka mali. Baadhi ya wachungaji wanapenda mambo ya dunia kuliko wanavyompenda Mungu. Baadhi yao huachana na huduma, lakini wengine hudiriki kuitumia huduma kama njia ya kujipatia mambo ya dunia hii.

Tabia ya waalimu wa mafundisho ya imani potofu ni kwamba wanafanya hivyo kwa ajili ya kujipatia mapato ya fedha (Tito 1:11; 2 Petro 2:3).

► Mwanafunzi atapaswa kusoma 2 Wakorintho 12:17-18 kwa ajili ya kikundi. Je, tunajifunza nini kuhusiana na Paulo na Tito kutoka katika kifungu hiki?

► Mwanafunzi atapaswa kusoma Wafilipi 2:19-22 kwa ajili ya kikundi. Je, tunajifunza nini kuhusiana na Timotheo kutoka katika kifungu hiki?

Paulo aliweka mfano wa kutumika kwa sababu ya upendo wake kwa Mungu. Timotheo na Tito walifuata mfano wake (Wafilipi 2:19-22; 2 Wakorintho 12:17-18).

Uwajibikaji Kifedha

Ni jambo la muhimu sana kuwa na uwajibikaji kwenye mambo ya kifedha katika kanisa la mahali au mtaa. Mtume Paulo aliweka mfano kwa ajili yetu. Alipokuwa akikusanya fedha kutoka katika kanisa moja na kupeleka katika kanisa lingine, aliweka watu wa kushuhudia na akahakikisha kwamba hakuna jambo lolote lililokuwa linafanyika kwa siri (2 Wakorintho 8:20-21).

Watu wa dunia hawawaamini watu wanaoshughulika na utunzaji wa fedha. Wanahisi kwamba watu wengi wanadokoa kutoka katika fedha wanazozitunza. Wanaamini kwamba wachungaji wengi wanatumika tu kwa ajili ya kujipatia mapato ya kifedha. Ni jambo la muhimu sana kwa kanisa la mahali kuwa na mfumo wa uwajibikaji wa kifedha ambao unathibitisha kwamba mchungaji wao anaweza akaaminika.

► Je ni mambo gani ya kufanya ambayo yatalisaidia kanisa kuonyesha kwamba mapato ya sadaka yanatumika kwa uaminifu?

Kwa ajili ya uwajibikaji kifedha, mapato ya sadaka yanapaswa yakusanywe na yahesabiwe na baadhi ya watu kwa pamoja, na siyo mtu mmoja tu. Mtu mwingine tofauti na si mchungaji atapaswa awe akiweka kumbukumbu za jinsi ambavyo fedha zinatumika.

Baadhi ya wachungaji hufundisha kwamba matoleo yote ya zaka ni mali yao. Biblia haijafundisha kwamba zaka yote inapaswa liende kwa mchungaji. Zaka hutumika kwa ajili ya makusudi mbalimbali (Kumbukumbu la Torati 26:12).

Mchungaji atapaswa kusaidia katika kusimamia matumizi ya zaka na sadaka mbalimbali kwa ajili ya kutunza huduma ya kanisa. Kusanyiko la kanisa litakuwa tayari kutoa zaidi kama litaona kwamba kuna uaminifu kwenye matumizi ya sadaka mbalimbali wanazotoa.

Taarifa Saba kwa Muhtasari

1. Huduma kwenye eneo jipya inapaswa kusisitiza injili na kuwavutia watu walio sahihi.

2. Kanisa lililokomaa siyo tegemezi kwa misaada ya nje au kwa uongozi.

3. Mashirika yanapaswa yasaidie makanisa katika njia ambayo haitadhoofisha msaada kutoka mahali pale pale.

4. Mashirika yanayotoa ufadhili mara nyingi yanakwamisha huduma za kanisa na kusababisha kanisa kuwa tegemezi.

5. Kanisa linapaswa kumtegemeza mchungaji wao ili aweze kutoa muda wake mwingi kwa ajili ya huduma ya kanisa.

6. Kanisa linapaswa liwe na mfumo wa uwajibikaji ambao utathibitisha uaminifu wao.

7. Mchungaji anapaswa kuhamasishwa na upendo wake kwa Mungu na kutaka sana kutumika.

Kazi za kufanya Somo la 8

1. Kariri taarifa Saba kwa Muhtasari kwa ajili ya somo la 8. Andika aya moja inayoelezea maana na umuhimu wa kila kipengele katika hizi Taarifa Saba kwa Muhtasari (jumla aya saba) kwa mtu ambaye siyo wa darasa lako. Wakilisha kwa kiongozi wako wa darasa kabla ya kuanza kwa kipindi cha darasa kinachofuata. Kuwa tayari kushirikisha aya moja kwa kikundi kama kiongozi wa darasa atakutaka ufanye hivyo wakati wa majadiliano. Andika taarifa hizi kutoka kwenye ufahamu wako bila ya kuangalia mahali popote mwanzoni mwa kipindi cha darasa kinachofuata.

2. Kumbuka kutengeneza ratiba ya nafasi yako mwenyewe ya kufundisha kwa wakati ambao utakuwa nje ya darasa na utoe mrejesho wako kwa kiongozi wa darasa baada ya kuwa umemaliza kufundisha.

3. Mtihani: Kwenye mwanzo wa kipindi kingine cha darasa, unahitajika kuandika kutoka katika kumbukumbu za ufahamu wako bila kukariri angalau sababu tano kutoka katika sababu sita zinazofanya kanisa liweze kupata msaada wa mahali pale pale na sera nne za kifedha za umisheni.

Next Lesson